Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Demokrasia Iko Zaidi ya Uchi Nchini Kenya

Na: Ali Nassoro*

Wakenya hivi majuzi pasi na shaka yoyote walishuhudia kufichuka kwa demokrasia  zaidi ya maelezo kiasi ya kuwa hata watetezi wenyewe wa demokrasia walipigwa na bumbuazi wasijue pa kuficha nyuso zao pindi sura halisi ya demokrasia ilipojitokeza wazi kinyume na matakwa yao na njama zao za kuiziba.

Yafuatayo ni baadhi ya matukio muhimu yaliyofichua umbile hadaifu la demokrasia, inayopigiwa debe na Wamagharibi kama kilele cha mafanikio ya wanadamu katika utawala:

Kwanza: Uhuru wa Kisanii wa Mikono ya Serikali na Tume za Kikatiba ulifichuka kikamilifu na kuwekwa mateka kama ilivyo tarajiwa kwa kuwa baraza la mawaziri ndilo pekee lenye mamlaka katika dola za kidemokrasia huku mikono mengineyo ya serikali na tume za kikatiba kwa ujumla zikitii maagizo ya baraza la mawaziri. Maafisa wanaohudumu katika taasisi hizo tiifu daima huegemea matakwa ya baraza la mawaziri.

Katika Upande wa Mahakama, matukio yafuatayo yalijitokeza:

1. Mahakama ya Upeo ya Kenya ilishindwa kutimiza kiwango cha idadi ya majaji kuweza kusikiza kesi yenye maslahi makubwa kwa umma. Hii imejitokeza kutokana na kuwa siku moja kabla mnamo 24 Oktoba 2017 baraza la mawaziri kupitia Kaimu Waziri wa Usalama wa Ndani lilitangaza tarehe 25 Oktoba 2017 kuwa siku kuu ya umma. Hili lilimfanya Jaji Mkuu aliye pia Raisi wa Mahakama ya Upeo kupeana mamlaka kwa majaji wa kitengo cha katiba na marekebisho ya mahakama mnamo 25 Oktoba 2017 kuketi na kuamua mambo yanayo husiana na uchaguzi wa uraisi wa tarehe 26 Oktoba 2017.    

2. Mahakama ya Rufaa ilikataa kutoa uamuzi kwa mambo yaliyo wasilishwa mbele yake majira ya asubuhi na kusema kwamba iko likizoni, lakini; baadaye ikajitokeza majira ya usiku na kutoa uamuzi wa kusitisha hukumu iliyotolewa mapema na Mahakama Kuu. Walisema kadhia iliyoko mbele yake ilikuwa ya dharura na hivyo basi kuwataka wao waketi majira ya usiku!

Katika Upande wa Bunge, tukio lifuatayo lilijitokeza:

1. Wabunge walipitisha marekebisho kwa sheria za uchaguzi za Kenya yaliyo idhinishwa na baraza la mawaziri yatakayo zivunja nguvu za Mahakama na Tume ya IEBC.

Katika Upande wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), matukio yafuatayo yalijitokeza:

1. Mwenyekiti wa Tume ya IEBC mnamo 18 Oktoba 2017 alisema kwamba hawezi kudhamini uchaguzi wa haki na kwamba yuko katika hali ya usumbufu kutoka kwa makamishna wenzake ambao daima humpiku katika maamuzi yoyote. Alitaja kuwa mateka kutokana na baadhi ya wanachama wa idara utekelezaji kukataa kujiuzulu baada ya kutajwa kwa mapana kuhusika katika uchaguzi ulio batilishwa na kuahidi kujiuzulu endapo mapendekezo yake hayata shughulikiwa. Haya yalijiri siku hiyo hiyo ya kujiuzulu ghafla kwa Dkt. Roselyn Akombe mmoja wa makamishna wa Tume ya IEBC akitaja kubughudhiwa kuwa miongoni mwa makamishna wenza ambao wamekuwa wakichukua maamuzi yao kutoka kwa baraza la mawaziri. Mwenyekiti wa Tume alisonga mbele na kumtaka Raisi na kiongozi wa upinzani kukutana naye afisini mwake katika jumba la Anniversary Towers. Cha kustaajabisha ni kuwa kiongozi wa upinzani Raila Odinga aliitika mwito huo na kwenda kukutana na mwenyekiti wa Tume ya IEBC afisini mwake katika jumba la Anniversary Towers mnamo 19 Oktoba 2017, lakini; Raisi alikataa na badala yake mwenyekiti wa IEBC yeye ndiye aliyekwenda kukutana na Raisi afisini mwake jumba la Harambee mnamo 23 Oktoba 2017.  

2. Mwenyekiti wa IEBC alibaki kimya na kisha kuibuka na kutoa taarifa mnamo 25 Oktoba 2017 kwamba uchaguzi utaendelea licha ya kuwepo na miito ya kuususia kutoka kwa kinara wa upinzani. Taarifa hiyo haikueleza kuhusu kadhia alizozitaja katika taarifa yake ya mnamo 18 Oktoba 2017 ikiwa zimeshughulikiwa au la. Hili likadhibitisha kikamilifu kuwa ni mtu alitekwa mateka na anakabiliwa na shinikizo kutoka kwa baraza la mawaziri kuendelea na kusimamia uchaguzi wa uraisi katika hali yoyote ile.

3. Licha ya uamuzi wa Mahakama Kuu mnamo 24 Oktoba 2017, kwamba Raila Odinga hawezi kushurutishwa kushiriki uchaguzi na baada ya kupokea barua rasmi kutoka kwa mgombea uraisi wa NASA kuwa yeye na mgombea mwenza wamejiondoa kutoka kwa uchaguzi ujao wa uraisi wa 26 Oktoba 2017 bado waliendelea na uchapishaji wa karatasi za uchaguzi yakiwa na jina la mgombea uraisi wa NASA.

Pili: Matakwa maarufu ya watu hayawasilishwi na maamuzi ya walio wengi, bali na maamuzi ya wachache kama ilivyo dhihirishwa na uchaguzi wa uraisi ulio kamilika hivi punde. Pindi kinara wa upinzani alipotoa wito kwa wafuasi wake sugu kususia marudio ya uchaguzi wa uraisi mnamo 26 Oktoba 2017 huku Raisi – kinara wa Jubilee akitoa wito kwa taifa kushiriki katika uchaguzi ujao. Idadi ndogo ya wapiga kura ilishuhudiwa hata katika maeneo yanayo julikana kuwa ngome za Jubilee halikuwashangaza tu muungano tawala wa Jubilee bali pia waangalizi wa humu nchini na wa kimataifa na hata kuvigawanya vyombo vya habari vya humu nchini na vya kimataifa vikikadiria kuwa idadi ya waliojitokeza ni asilimia 34% na 27% mtawalia. Hii yamaanisha kuwa idadi kubwa ya watu wamekataa kushiriki katika uchaguzi wa uraisi uliokamilika hivi punde lakini 'demokrasia' inashikilia kwamba waliopiga kura wametoa sauti zao na kwamba sauti zao ndizo zitakazo amua matokeo ya uchaguzi huu na mwelekeo wa nchi.

Tatu: Msemo kuwa kutopiga kura ni haki ya kidemokrasia na kwamba idhaminiwe sio kweli kama ilivyo thibitishwa na marudio ya hivi punde ya uchaguzi wa uraisi ambapo wengi wa walio sajiliwa kupiga walisusia na haki yao haiku dhaminiwa kama ilivyo ahidiwa. Kwani wote ambao hawakupiga kura ni wengi ikilinganishwa na waliopiga na hivyo basi ilitarajiwa kuwa ushindi wa uchaguzi huu ungekuwa kwa walio ususia. Badala yake demokrasia 'inapeana uzito' kwa wengi waliopiga kura na sio waliosajiliwa kupiga kura ambao hawakushiriki katika kuupa uchaguzi imani na kuuhalalisha utawala. Hivyo basi mshindi kwa kutumia akili makini ni waliosusia uchaguzi lakini katika demokrasia ni wale ambao walishiriki.

Nne: Kushiriki katika uchaguzi wa kidemokrasia sio jambo la dharura kwa maendeleo ya kisiasa pamoja na ya kijamii na kiuchumi kama ilivyo daiwa mwanzoni na Ummah wa Kiislamu. Hili limethibitisha lengo halisi la chaguzi za kidemokrasia kama njia ya kufikia utawala kwa kutumia watu kama mashini za kupigia kura kuthibitisha na kuhalalisha serikali mpya au iliyoko. Kwa mfano Ummah wa Kiiislamu ambao kwa muda mrefu umeonywa dhidi ya kushiriki katika chaguzi za kidemokrasia kwani demokrasia yenyewe ni nidhamu ya utawala itokanayo na mfumo batili wa kirasilimali. Itikadi ya mfumo huu wa kirasilimali – ilmaniya, hutenganisha dini na serikali; hivyo basi, huwapa wanadamu mamlaka ya kujitungia sheria wenyewe zitokanazo na akili zao finyu. Hilo hugongana na itikadi ya Kiislamu inayo walingania waja kujisalimisha kikamilifu kwa sheria zilizo teremshwa na Muumba. Kwa hivyo, kipimo cha vitendo vya wanadamu kimejengwa juu ya halal na haram pekee na kwamba ikiwa wanadamu wanataka kususia au kushiriki katika jambo lolote ni lazima wajenge juu ya msingi huu na wala si msingi mwengineo ulio vuliwa kutoka kwa mfumo batili wa kirasilimali. Hivyo basi Ummah wa Kiislamu unatakiwa kuitikia na kutenda anayo walingania Allah (swt), na sio kuitikia yale wanayo yalingania viongozi wa kidemokrasia ima wawe ni Waislamu au si Waislamu ya kushiriki au kususia matukio/michakato fulani kwani kumuitikia Allah hudhamini kuingia Jannah huku kuwaitikia viongozi hawa hudhamini Jahannam. Bila ya kujali yale yatakayo jitokeza yakiwemo maumivu, kupotea au kupatikana kwa mali kinacho stahili kuupa motisha Ummah wa Kiislamu ni kuitikia na kutenda aliyolingania Allah (swt).

Enyi Wanadamu jiepusheni na demokrasia kwa sababu hakika siyo inayo dhamini amani, utulivu na maendeleo kwa kuwa inatokamana na akili finyu ya mwanadamu na ambayo huathiriwa na mabadiliko kulingana na dhurufu. Badala yake kumbatieni Uislamu kama mfumo badili na kamilifu kutatua matatizo yanayo ikumba Kenya na kila sehemu ulimwengu. 

Enyi Ummah wa Kiislamu imeharamishwa kuitekeleza au kuilingania demokrasia kwa sababu ni nidhamu batili inayopigiwa debe na Mmagharibi. Kamwe haina uhusiano wowote na Uislamu. Inagongana kikamilifu na hukmu za Kiislamu ima katika kadhia jumla au maalum, kutokana na chimbuko lake, kutokana na 'Aqeedah inayo chipuza kwayo, kutokana na msingi ulio jengwa juu yake na kutokana na fikra na nidhamu ilizo leta.

* Imeandikwa kwa Ajili ya Gazeti la Ar-Rayah - Toleo 155

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumamosi, 18 Aprili 2020 15:51
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.