Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Lengo la Mwanasiasa wa Kidemokrasia ni Kujinufaisha Binafsi na Sio Kuwatumikia Raia

Habari:

Kumekuwa na mjadala unaoendelea nchini kuhusu utofauti mkubwa wa viwango vya mishahara kati ya wanasiasa na watumishi wa umma. Wakati wanasiasa wanalipwa mshahara mkubwa na mafao manono, wafanyakazi wengine wanatolewa kafara kwa kupewa mshahara wa ‘kijungu mwiko’ (ya chakula cha siku) huku wakikabiliwa na makato makubwa ya kodi. (BBC Swahili 17/07/2020)

Maoni:

Hali hii inathibitisha ukweli kwamba viongozi wa kidemokrasia wapo kwa ajili ya maslahi yao binafsi na si kwa maslahi ya watu waliowachagua. Mbunge nchini Tanzania hulipwa mshahara wa Tsh milioni 3.8, na posho ya Tsh milioni 8 kila mwezi (takribani dolari 5,130), kuna posho ya kila kikao Tsh 240,000, posho ya kujikimu Tsh 120,000, kiinua mgongo Tsh milioni 240 baada ya miaka mitano, bima ya afya ya daraja la kwanza kwake na familia yake nk.

Kwa upande mwingine, mfanyakazi wa serikali ambaye ni muhitimu wa shahada ya kwanza (digrii)) analipwa mpaka Tsh 733,000 (takriban dolari 318) kwa mujibu wa ngazi za mshahara za serikali (TGSTD1). Hii inamaanisha kuwa mshahara wa mfanyakazi mwenye shahada ya kwanza kwa mwaka mzima haufikii mshahara wa Mbunge wa mwezi mmoja pamoja na marupurupu yake.

Hapana shaka hii ndio sababu inayofanya wataalamu kuhama katika utumishi wa kawaida wa serikali na kukimbilia vyeo vya kisiasa kwa lengo la kujipatia maslahi makubwa zaidi (malisho ya kijani)

Kama wanasiasa hawa wangekuwa kwa ajili ya watu kama wanavyodai, wasingekubali utofauti huu mkubwa kati yao na watu wao, unaowafanya waishi maisha ya anasa ilhali walio wengi wanataabika hawajui hata vipi watamudu walau mlo mmoja wa siku.

Zaidi ya hayo, licha ya kuwa mshahara wanaopata wafanyakazi wengine wa serikali kuwa mdogo (ili mradi mkono uende kinywani) bado umesheheni makato na kodi za kinyonyaji kama kodi ya mapato, mifuko ya hifadhi ya jamii, vyama vya wafanyakazi, mkopo wa elimu ya juu, bima ya afya nk.  ambavyo kiujumla huweza kufikia mpaka 30% ya mshahara. Wakati wengine wakiwa na makato kama hayo, mishahara ya wanasiasa haina makato hayo, mfano mzuri ni huo mshahara wa mbunge.

Huu ni ukweli wa wazi wa demokrasia, viongozi wa kidemokrasia na ubepari kiujumla, wanasiasa hawajali maslahi ya watu, wanawatumia tu kujitajirisha wao na kuridhisha mabwana zao wakoloni wamagharibi.

Chanzo kikuu cha unyonyaji huu iwe Tanzania, Afrika na ulimwenguni kote kiujumla ni kukataa sharia za Muumba na badala yake kiumbe ambaye ana ukomo wa kufikiri amepewa nafasi ya kutunga sheria kusimamia wenzake.

Kwa kuwa wanadamu ni wabinafsi kiasili, wakitawaliwa na fikra zao binafsi na matamanio yao daima  watatunga sheria zenye kuwalinda wao, familia zao na marafiki.  Zaidi ya yote haitarajiwi binadamu kutunga sheria itakayotumikia ubinadamu kwa haki.                                                                          

Katika Uislamu chini ya dola ya Khilafah wote waliopewa nyadhifa za kisiasa (ambao huwa wachache) hawana nafasi ya kujinufaisha katika nidhamu isipokuwa kutumikia watu, watapewa malipo yatakayowawezesha kupata mahitaji yao.

Kuhusu suala la ajira na mishahara, huwa ni makubaliano kati ya mwajiri na mwajiriwa kulingana na thamani ya kazi. Mkataba wa ajira ni kati ya mwajiri na mwajiriwa, hakuna makato ya vyama vya wafanyakazi, hakuna kodi ya mapato, hakuna makato ya bima ya afya, kwa vile dola ya Khilafah itadhamini huduma bora za afya bure au kwa malipo hafifu sana.

Imeandikwa Kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa
Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumatatu, 25 Januari 2021 13:05
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.