Logo
Chapisha ukurasa huu

Afisi ya Habari
Wilayah Misri

H.  14 Jumada II 1444 Na: 1444/07
M.  Jumamosi, 07 Januari 2023

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Mgogoro wa Kiuchumi wa Misri, kwa kweli, ni Mgogoro wa Kimfumo

Ndio Mzizi wa Maradhi na Chanzo cha Mateso
(Imetafsiriwa)

Umaskini uliokithiri, ukosefu wa ajira uliogubika, machafuko ya kisiasa na kiuchumi, utajiri wa kupindukia kwa wachache kwa gharama ya watu wengi, kushuka kwa thamani ya pauni dhidi ya fedha za kigeni kusikokuwa na kifani, kula akiba za watu, kushuka kwa kiwango kikubwa cha maisha, kuongezeka kwa kasi kwa deni la umma, kupanda kwa bei kusiko na kifani, kupuuza rasilimali za kiuchumi na kimkakati kwa ajili ya maadui wa Ummah... ni uhalisia ambao Misri inaishi siku hizi. Mgogoro wa kiuchumi umezidi kuwa mbaya katika miaka ya nyuma baada ya jeshi kunyakua utawala na mamlaka, licha ya kwamba sababu iliyotangazwa ya mapinduzi ya jeshi dhidi ya Mohamed Morsi ilikuwa ni kuinusuru nchi hiyo isiporomoke na kuzuia kuuzwa kwa uwezo wake kwa Qatar!

Inashangaza kwamba hakuna suluhu za kweli zinazopendekezwa na utawala huo ili kujiondoa katika mgogoro huo, na inachotoa ni sera za kifisadi, kama vile kukopa kutoka kwa Mfuko wa Fedha wa Kimataifa na Benki ya Dunia, ambazo zimeitumbukiza Misri kwenye dimbwi la mrundiko wa madeni na riba maradufu tangu miaka ya sabiini ya karne iliyopita. Mikopo hii inatolewa na taasisi hizi mbili za kimataifa za kikoloni chini ya masharti makali. Uchumi wa Misri umewekwa rehani kwa utashi na ulafi wa dola za kikoloni, na masharti haya hayajawahi kuipelekea nchi yoyote katika mwamko wa kweli wa kiuchumi. Badala yake, yamesababisha ongezeko la kodi na kuondolewa kwa ruzuku kwa bidhaa za kimsingi, na kile wanachokiita katika kamusi zao "kusawazisha matumizi" ili kuwafanya watu kuwa maskini na maskini zaidi.

Utawala wa Misri unasisitiza kuzunguka katika duara baya la madeni, kujaza madeni ya riba kwa madeni mapya. Mfuko wa Fedha wa Kimataifa hivi majuzi ulikubali kutoa mkopo mpya wa dolari bilioni 3 kulipwa kwa muda wa miezi 46, na kuifanya Misri kuwa nchi ya pili yenye deni kubwa la mfuko huo baada ya Argentina. Benki Kuu ya Misri pia ilipandisha viwango vya riba kwa pointi 300 (3%), ikidai kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya kukabiliana na kuzorota kwa pauni ya Misri, na hivyo kusimamisha ongezeko la kasi ya mfumko wa bei ambao umefikia 19%, na kwa mujibu wa ripoti ya Benki Kuu ya Misri kwa mwezi wa Septemba 2022, deni la nje la nchi hiyo lilifikia takriban dolari bilioni 157.8. Hii inamaanisha ongezeko la takriban mara 5 ikilinganishwa na miaka kumi iliyopita, kwani lilifikia takriban dolari bilioni 34.4 mwishoni mwa 2012.

Jaribio baya la serikali kutaka kutoka katika handaki hili la giza kupitia kukopa, kuongeza kiwango cha riba, na kuuza mali ya serikali, halitafanikiwa, kwani yote ni suluhu zilizochukuliwa kutoka kwa mfumo wa kibepari, ambao ndio msingi wa mateso. Mfumo huu, pamoja na taratibu zake, sheria, na uhuru wake wa kifedha, uzipa uhuru wa kutawala taasisi za kishetani za mabepari na walanguzi kuhodhi pesa nyingi zaidi na kukuza utajiri wao kwa gharama ya umma jumla. Kwa hiyo sababu ya kufeli kwa masuluhisho na mipango yote hii katika kufufua uchumi na kuondokana na mgogoro ni kwamba yanachukuliwa kutoka kwa mfumo huu uliounda na kusababisha mgogoro huu. Kwa hivyo anayetafuta ulinzi kutokana nao, ni kama mtu anayejikinga kutokana na joto kali kupitia moto. Wanafikra wa Kimagharibi na mabepari wakuu wenyewe walitilia shaka ufanisi wa masuluhisho yaliyopendekezwa, na walikiri kwamba masuluhisho haya - endapo yatafanikiwa - yangechangia tu kuakhirisha kuanguka, lakini kutatua matatizo kwa ufumbuzi msingi, hili halitakuwa.

Sisi katika Hizb ut Tahrir tunatoa wito wa suluhisho la mgogoro huu kupitia mabadiliko msingi. Suluhisho haliwezi kutoka ndani ya mtikisiko wa uchumi wa kibepari ambao ulisababisha kuzorota kwa uchumi. Badala yake, kuta za kifikra ambazo kwazo zimetuzingira lazima zivunjwe na kutafuta suluhu kutoka nje yake. Hivi ndivyo ilivyo kwa kila mfikiriaji na mwanasayansi anayetafuta suluhisho la kweli kwa matatizo yoyote. Sisi, kama chama cha kisiasa, tunauelewa Uislamu kama mfumo mpana wa maisha ambao kwao nidhamu zote huchipuza ambazo huyaongoza maisha ya mwanadamu katika ulimwengu huu kwa njia sahihi na ya kipekee. Tunatoa wito kwa wanadamu wote kuusoma Uislamu na mfumo wake wa kiuchumi kwa uchunguzi wa kina na mpana, ili kutafuta utukufu wa Uislamu na utukufu na usahihi wa masuluhisho unayoyatoa, na watambue kuwa huo ndio mfumo pekee unaomiliki masuluhisho sahihi kwa matatizo yake, na kwamba hakuna mwokozi wala afueni isipokuwa kwa kuutekeleza kikamilifu katika mambo yote ya maisha.

Inasikitisha sana kwamba sisi Waislamu, wamiliki wa mfumo huu mtukufu wa Mwenyezi Mungu, katika kutatua matatizo yetu katika ardhi ya Kinana, tunakimbilia kwenye mifumo mibovu uliyotungwa na watu, ambayo kufeli kwake kumethibitika mbele ya wengine, na tunapaswa kurudi kwenye Uislamu wetu mtukufu kuufahamu na kuufanya kuwa msingi wa kutatua matatizo yetu yote. Inatutosha sisi kauli ya Mola Mlezi, Mwenye baraka na Aliyetukuka, katika Kitabu chake.

(وَلَوْ أَنَّ أَهْلَ الْقُرَى آَمَنُوا وَاتَّقَوْا لَفَتَحْنَا عَلَيْهِمْ بَرَكَاتٍ مِنَ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ وَلَكِنْ كَذَّبُوا فَأَخَذْنَاهُمْ بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ)

“Na lau kuwa watu wa miji wangeli amini na wakamchamngu, kwa yakini tungeli wafungulia baraka kutoka mbinguni na katika ardhi. Lakini walikanusha basi tukawapatiliza kwa sababu ya yale waliyo kuwa wakiyachuma.” [Al-Araf: 96].

Uchamungu wa kweli ni kwamba tumche Mwenyezi Mungu katika kila jambo tunalolifanya, yaani tunashikamana na maamrisho yake, Mola Mtukufu, na kuepuka makatazo yake katika yale tunayoyafanya ya amali, ikiwemo miamala yote katika nyanja za kiuchumi, hivyo tunajitolea kuingia mikataba, kununua na kuuza, kuanzisha makampuni, na shughuli zote za kibiashara kwa mujibu wa hukmu za Sharia kwa ukamilifu, na Sharia imeeleza kwa undani wa kutosha, na kuweka masharti makali kwa shughuli zote za kibiashara. Ni makosa makubwa kudhani kuwa mfumo wa uchumi katika Uislamu ni sawa na mfumo wa kibepari, lakini bila riba, kwa sababu misingi ambayo mfumo wa uchumi katika Uislamu umeegemezwa ni tofauti kabisa na ule ambao mfumo wa kibepari umeegemezwa. Kuna aina za umiliki ambazo huamuliwa na asili ya kitu kinachomilikiwa, kwa hivyo ima ni umiliki wa mtu binafsi, umiliki wa umma, au umiliki wa serikali na kuna vitu ambavyo umiliki wake hauruhusiwi kibinafsi kabisa, sio kwa kampuni au kwa watu binafsi (kama vile visima vya mafuta na gesi na utajiri usio malizika ardhini), na mgawanyo huu haufafanuliwi na mfumo wa kibepari, kama ambavyo hakuna uhuru wa kumiliki katika Uislamu, lakini umiliki umewekewa mipaka kwa sababu tano zilizoainishwa na Ash-Shari’, tofauti na ubepari ambao umeruhusu umiliki kwa njia yoyote ile, mradi hauingilii haki za wengine, iwe kwa riba, kamari, uasherati, na kadhalika. Katika sekta ya makampuni, Uislamu umeharamisha makampuni ya fedha peke yake, kama vile makampuni ya hisa, ambayo ndani yake ombi (Ijab) na kukubali (qabul) hazipo na ile sifa ya kihakika haipo kwazo, na umeharamisha mtu kuuza asichomiliki; kwa vizuizi hivi vya kisheria na mengineyo, mfumo wa kiuchumi wa Kiislamu umeegemezwa juu yake, ambao huzalisha masuluhisho ya matatizo yote ya kiuchumi katika dola ndani ya mfumo kamili wa Kiislamu katika utawala, sera ya kigeni, mfumo wa elimu, mfumo wa kijamii nk. Hii ni kwa sababu ni muundo uliounganishwa, sio muundo wa viraka kutoka kwa kila kipande! Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba mgogoro wa sasa wa kiuchumi nchini Misri ni mgogoro wa mfumo. Kwa hiyo, ni lazima utamkwe kama kiini, na Uislamu lazima utekelezwe kivitendo katika mapinduzi ya haraka na ya kina.

Enyi Wanyofu katika Jeshi la Kinana: Enyi mliobeba katika nyoyo zenu mapenzi ya Mwenyezi Mungu, Mtume Wake, na Dini yake, ni yupi aliye kwa ajili ya Uislamu, sheria yake, na dola yake, ikiwa si nyinyi?! Nani mwengine atakayeunusuru?! Nyinyi ndio wajuzi zaidi katika watu kuhusu ufisadi wa utawala huu, raia wake na watekelezaji wake. Hili linashuhudiwa kwa mishahara na marupurupu munayopewa, kama rushwa ambayo kwayo kimya chenu kinahakikishwa, upande wenu unaaminiwa na uaminifu wenu unanunuliwa. Na ni kidogo sana kuliko haki zenu halisi kutoka katika mali ya Misri na neema kubwa, hivyo msiwabadilishe watawala kwa yale aliyokuhalalishieni Mwenyezi Mungu, yatakayokutumbukizeni na watoto wenu katika shimo la Jahannam, na vueni ukosi wa utawala huu kutoka shingoni mwenu na mukate kamba zote zinazokufungeni nao, na chukueni upande wa familia yenu na mutimize azma yao ya maisha ya staha. Inaweza tu kupatikana kupitia Uislamu na dola yake. Dola ya Khilafah Rashida kwa njia ya Utume, basi kuweni Answari (wanusuru wake), na regesheni urithi wa Answari wa jana kwa kuinusuru Hizb ut Tahrir ili kuisimamisha, Mwenyezi Mungu akupeni ufunguzi na kukamilisha baraka na fadhila zake juu yenu, ili Misri iwe ngome ndani yenu, Misri yenye nuru, kito cha thamani cha taji la Khilafah na nguzo yake, Ewe Mwenyezi Mungu, ijaaliye iwe mapema zaidi kuliko baadaye.

Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir
katika Wilayah Misri

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Wilayah Misri
Address & Website
Tel: 

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.