Logo
Chapisha ukurasa huu

Afisi ya Habari
Tanzania

H.  27 Jumada I 1443 Na: 1443 / 02
M.  Ijumaa, 31 Disemba 2021

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Taasisi za Fedha za Kimataifa Zinafanyia Kazi Ajenda ya Kiunyonyaji

Katika kipindi kisichozidi mwaka mmoja tangu kushika mamlaka ya uraisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Samia Suluhu tayari serikali imeshachukua mkopo wa kiasi cha billioni $3 ikihusisha kinachoitwa mifuko ya mikopo yenye takhfifu na pia kutoka katika mfuko wa kujifariji na majanga kutoka Benki ya Dunia, Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Benki ya Dunia pekee imeikopesha Tanzania mkopo wa kiasi cha billioni $2.29 kwa ajili ya miradi mbali mbali ikiwemo millioni $500 kwa ajili ya kutoa msukumo wa Mpango wa Masomo ya Elimu ya Msingi, millioni $150 kwa ajili ya Mradi wa Kuimarisha Umilikishaji Ardhi (LTIP) na millioni $500 kwa ajili ya Mradi wa kuboresha Kiwango cha Elimu ya Sekondari Tanzania.

Nayo IMF iliidhinisha kiasi cha millioni $567 kwa Tanzania, miongoni mwao millioni $189 kutoka chini ya Mpango wa Mikopo ya Kiharaka na millioni $378 chini ya Mpango wa Ufadhili wa Kiharaka.

Pia, Tanzania imechukua mkopo wa kiasi cha millioni $256 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika, huku kiasi cha millioni $140 kikilengwa kutumika katika uzalishaji wa nishati ya umeme na mtandao wa uunganishaji wake, ilhali kiasi cha millioni $116 kitatumika kwa ajili ya maboresho makubwa ya barabara ya kilomita 160 inayounganisha Mnivata- Newala na Masasi, kusini mwa Tanzania.

Tanzania kama zilivyo nchi nyengine za Afrika imekuwa ikikopa kutoka kwa taasisi hizo za kimataifa kwa miaka mingi tu, wala hakuonekani dalili ya kusita wala hali ya kujisimamia mambo yake kwa kuwa huru kutokana na madeni na ukopaji huo.

Mfano hai, ndani ya mwaka 2015, deni la Tanzania lilkuwa trillioni 35 na hadi kufikia Aprili 2021 limeshapaa kufikia trillioni 60.9. Hali hiyo imejiri kutokana na kuchukua mikopo kutoka kwa taasisi hizo za kifedha za kimataifa.

Tangu Marekani itamalaki kimataifa baada ya Vita vya Pili vya Dunia iliasisi mpango mpya kabambe wa kudhibiti uchumi kufuatia Mawafikiano ya Bretton Woods ndani ya mwaka 1944, kutokana nayo iliundwa Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), taasisi mbili hizo zikiwa ala muhimu za Marekani kudhibiti uchumi, ikizitumia kama kadi yake ya kuchezea uchumi, na baadhi ya wakati kupitia mikopo ili kuondoa tawala ambazo awali zilikuwa vibaraka wa mabwana wa ukoloni mkongwe (Uingereza na Ufaransa) na kuzibadilisha tawala hizo kuwa vibaraka wake wapya. Pia taasisi mbili hizo hutumika kuwa na udhibiti kikamilifu wa uchumi wa nchi mbali mbali kupitia makampuni ya Marekani ya kimataifa, ikipelekea wizi wa vyanzo vya uchumi vya nchi mbali mbali kwa kubadilisha mali za Umma kuwa za kibinasi chini ya ajenda yake ya ubinafsishaji nk.

Kwa hivyo, taasisi zote za kifedha za kimataifa iwe Benki ya Dunia, IMF, za Ulaya, za China au hata Benki ya Maendeleo ya Afrika iliyoasisiwa mwaka 1964, zote hizo si chochote si lolote ila kimaumbile ni taasisi za kibepari ambazo kamwe hazikudhamiriwa kuisaidia Afrika au nchi zinazoendelea. Lakini kimsingi zina ajenda ya kiunyonyaji zikilazimisha kwa ukatili na bila ya huruma sera za kinyonyaji kama Sera ya kufanya mabadiliko ya kimuundo iliyoleta mashaka na maangamizi makubwa kwa uchumi na watu.

Kwa sasa inadhihirika wazi kwamba madeni ni ala ya kinyang’anyiro cha ukoloni mambo leo baina ya Marekani, Ulaya na China ili kutenza nguvu na kunyonya mrundikano mkubwa wa rasilimali za Afrika na utajiri wake kupitia baraka za  wanasiasa wa nchi zinazoendelea kwa gharama ya wananchi wanyonge ambao ndio wahanga wakubwa wa maumivu ya madeni hayo na wabebaji mzigo wa kodi ili kulipia madeni hayo. Katika baadhi ya nchi zinazoendelea wamefikia hatua ya kupoteza miundombinu yao nyeti kwa kushindwa kulipa madeni makubwa ya nje kwa wakati. Orodha ya nchi zilizosibiwa na hali hiyo ni ndefu, zikiwemo nchi kama Zambia, Uganda Sri Lanka nk.

Mataifa ya nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania lazima ziamke kwamba ulimwengu unahitaji mfumo wa uadilifu wa Uislamu ili kuwa na maamiliano ya kiuadilifu ya kiuchumi, na sio mfumo muovu na wa kiunyonyaji wa Ubepari. Uislamu chini ya utawala wake wa Khilafah utauokoa ulimwengu na ubinadamu kiujumla kutokana na minyororo yote ya kiunyonyaji.

Masoud Msellem

Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari

Hizb ut Tahrir Tanzania

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Tanzania
Address & Website
Tel: +255778 870609
E-Mail: mediarep@hizb.or.tz

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.