Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Umwagikaji Damu: Ni Nani wa Kulaumiwa?

Milipuko miwili iliyotikisa jiji la Mombasa na Nairobi wikendi iliyopita iliyowaua jumla ya watu sita na wengine kadhaa kujeruhiwa ni tukio la kuhuzunisha mno. Hili ni takribani mlipuko wa themanini katika misururu ya matukio ya milipuko tangu Majeshi ya Ulinzi wa Kenya (KDF) kukabiliana na Al-Shabaab mnamo 2011 nchini Somalia. Inahuzunisha sana kuwa maisha yasiyo na hatia yanapotea na damu inaendelea kumwagwa; kwa sababu ya matukio haya, harakati ya kisiasa ya Kiislamu Hizb ut Tahrir / Afrika Mashariki ingependa kutoa maoni yafuatayo:

Kila matukio haya na mfano wake yanapotokea, vidole vya lawama huelekezewa Waislamu hata kabla ya uchunguzi wa sawasawa kufanywa na yanayofuata baadaye huwa ni misururu ya misako ya polisi inayopelekea Waislamu wengi kukamatwa. Linalo sikitisha katika zoezi lote hili ni namna Waislamu wanavyo dhalilishwa na kunyanyaswa pasi na hata chembe ya afueni. Mfano wa kusikitisha kama ilivyo ripotiwa na tovuti ya nairobinews.nation.co.ke, mtoto mchanga wa miezi sita alikufa kwa sababu mamake hakuwepo kumpa uangalizi kwa kuwa alinyakuliwa na kufungiwa katika kituo cha polisi cha Kasarani wakati wa oparesheni ya polisi inayoendelea kwa jina "Usalama Watch". Vitengo hivi vya polisi kikiwemo kitengo cha kupambana na ugaidi (ATPU) hutekelezwa mauaji nje ya sheria pasi na kujali sheria ya Kenya wala ya kimataifa. Wanafikia hadi kupuza maamuzi ya mahakama wakidai kuwa magaidi huachiliwa huru baada ya bondi na kuwasilishwa kwa mdhamini, jambo ambalo lilipingwa vikali na hata Hakimu DK Maraga mnamo 24 Aprili 2009 katika uamuzi wake juu ya tukio la Kanisa la Kiambaa wakati wa ghasia za baada ya uchaguzi alipowakashifu polisi na upande wa mashtaka kwa kazi yao duni na kuilaumu idara ya mahakama. Hili laonyesha wazi ukosefu wa ushahidi kwa washukiwa na pia unafiki wa mwito wao wa kushikamana na hukmu ya sheria na idara huru ya mahakama.

Ni dhahiri kuwa utovu wa usalama nchini Kenya umeongezeka pakubwa hususan baada ya oparesheni "LINDA NCHI" iliyotekelezwa na KDF nchini Somalia. Baada ya kupelekwa KDF nchini Somalia, ripoti nyingi zilipeperushwa hewani zikidai kuwa majeshi hayo yameziteka ngome za Al Shabaab. Swali ni: Je, ni kwa nini basi Wakenya wasio na hatia wangali wanauawa? Tunafahamu fika kiwango cha utovu wa usalama kilivyo nchini Somalia lakini si kweli kuwa uvamizi wa kijeshi ndio utakaoleta amani ya kudumu nchini Somalia kwa sababu tayari majeshi ya kigeni kutoka magharibi yaani Amerika na Ufaransa na kutoka mataifa mengine yamo nchini Somalia na amani ya kudumu bado haijapatikana. Chanzo cha ukosefu wa amani nchini Somalia ni mvutano baina ya mataifa ya kimagharibi katika kuvuna rasilimali asili za Somalia. Ni muhimu mno kufahamu kuwa mataifa ya magharibi, hususan Amerika upande mmoja na Ulaya upande mwingine, yameigeuza Somalia kuwa uwanja wa vita ili tu kuvuna rasilimali za Somalia na zaweza kubakia pekee ndani ya Somalia kupitia kisingizio cha kupigana na ugaidi. Mataifa haya yanafahamu waziwazi mzigo wa gharama za vita na hayawezi kuzimudu kufikia wakati huu hivyo yanayalazimisha mataifa madogo kama Kenya; mataifa ambayo hata hayawezi kujimudu yenyewe kiuchumi kwenda vitani ikiwacha majanga kuwaangukia raia wao wasio na hatia.

Inasikitisha sana kuwaona viongozi wa Afrika ikiwemo Kenya kufuata mfumo huu wa kikoloni; mfumo ambao hata umewafanya viongozi hawa kuwa vigumu kuangalia matatizo ya raia wao, na kuwafanya kujiingiza katika vita kwa jina "vita dhidi ya ugaidi" wakiutuhumu Uislamu na Waislamu kana kwamba Uislamu ndio chanzo cha kuwepo kwa matatizo yao. Ukweli ni kwamba Afrika ndio bara pekee ambalo lingali linavunwa na mfumo fisidifu wa kimagharibi. Hapa nchini Kenya unyanyasaji wa wakoloni sio kitu kigeni kwani Waafrika wengi walibandikwa jina la magaidi kwa sababu tu walikuwa wanapigania ardhi zao dhidi ya wavamizi wa kikoloni. 

Amerika na washirika wake wamehisi tishio la kusimama tena Khilafah ili kuudhibiti ulimwengu hiyo ni baada ya kudhihiri kufeli kwa mfumo wa kirasilimali kutatua matatizo ya ulimwengu bali ukweli ni kwamba wenyewe ni sehemu ya tatizo.

Mwisho tungependa kusema waziwazi kuwa; Miongoni mwa mafunzo ya Uislamu ni kulinda damu ya asiye na hatia, hivyo vitendo vya kusikitisha ambavyo vilitokea wakati wa wikendi havipaswi kamwe kuhusishwa na Uislamu wala Waislamu. Hili liko katika historia kwani katika zama za Khilafah wasiokuwa Waislamu walilindwa na tamaduni zao kuheshimiwa. Mtume (saw) asema,

«مَنْ كَانَ عَلَى يَهُودِيَّتِهِ أَوْ نَصْرَانِيَّتِهِ فَإِنَّهُ لاَ يُفْتَنُ عَنْهَا»

"Yeyote ima Mkristo au Myahudi hatoingiliwa kati kuhusiana na imani yake."
Hivi ndivyo namna KHILAFAH inayokuja itakavyo simamia na kulinda usalama na amani ya raia wake bila ya ubaguzi.


Shabani Mwalimu
Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari wa Hizb ut Tahrir Afrika Mashariki

H. 9 Rajab 1435
M. : Ijumaa, 09 Mei 2014

Hizb-ut-Tahrir
Afrika Mashariki

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.