Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Jibu la Swali
Athari za Kisiasa nchini Afghanistan

(Imetafsiriwa)

Swali:

Mnamo 17 Julai 2021, mazungumzo ya ngazi ya juu yalitangazwa nchini Qatar kati ya ujumbe miwili wa ngazi ya juu, wawakilishi saba kutoka Taliban na ujumbe wa wanachama saba wa serikali [Afghanistan], kujadili maswala muhimu kati yao, baada ya Rais wa Amerika kutangaza mnamo Julai 8, 2021 kwamba uondoaji wa vikosi vyake kutoka Afghanistan utakamilika ifikapo tarehe 31 Agosti, na kuusongeza mbele kutoka tarehe ya makataa ambayo alikuwa ameweka hapo awali. Mafanikio ya harakati ya Taliban yamezingatiwa katika maeneo makubwa ya Afghanistan, yamefikia asimilia 85, kama ilivyotangazwa na harakati hiyo ... Kwa mujibu wa Mkataba wa Doha wa 2020, mazungumzo kati ya harakati hiyo na serikali yana jukumu la kufikia mbinu ya ugavi wa mamlaka ya kisiasa. Je! Taliban watachukua udhibiti wa serikali au watagawanya tu madaraka? Je! Amerika kweli itaondoka au ushawishi wake utaendelea?

Jibu:

Ili kufikia rai nzito zaidi juu ya mambo haya, tunazingatia yafuatayo:

1. Wakati Amerika ilipoanza kupanga kwa umakini kujiondoa kwake Afghanistan, tangu mwishoni mwa 2010 na mwanzoni mwa 2011, Amerika ilitaka kuanza mazungumzo na viongozi wakuu wa Taliban kwa umakini, na Pakistan kama msimamizi katika mazungumzo haya. Amerika ilijionyesha kubadilika kwa Taliban, kiasi ya kuwa mnamo 2014 mazungumzo yalisababisha kubadilishana kwa wafungwa. Wafungwa watano wa Taliban kutoka Ghuba ya Guantánamo waliachiliwa huru kwa mbadala wa Taliban kumwachilia huru Mmarekani mmoja, Private Beaudry Robert "Bowe" Bergdahl, ambaye alikuwa anashikiliwa mateka na Taliban ... Halafu maendeleo katika mazungumzo yalishika kasi chini ya wanaume wawili waliohudumu kwa muda mrefu katika mamlaka husika walizowakilisha. Mnamo 5 Septemba 2018, Zalmay Khalilzad aliteuliwa kama Mwakilishi Maalum wa Amerika wa Upatanishi wa Afghanistan, aliyepewa jukumu la kumaliza uvamizi wa kijeshi wa Amerika nchini Afghanistan. Ndani ya miezi miwili ya kuteuliwa kwa Khalilzad, tarehe 22 Oktoba 2018, Pakistan ilimwachilia huru Mullah Abdul Ghani Baradar, ambaye alikuwa anazuiliwa nchini Pakistan tangu kukamatwa kwake huko Karachi, kufuatia uvamizi wa tarehe 8 Februari 2010. Baada ya kuachiliwa huru, Mullah Baradar aliteuliwa kuwa mkuu wa afisi ya kidiplomasia ya Taliban jijini Doha. Habari za Kiarabu za BBC ziliripoti mnamo 25 Februari 2019, kwamba, "Jina la Mullah Baradar lilikuja juu ya orodha ya wafungwa ambaye harakati hiyo ilitaka kuachiliwa kwake, katika mazungumzo yake mfululizo na maafisa wa Amerika na serikali ya Afghanistan, hadi hatimaye kuachiliwa huru mnamo Oktoba 2018, baada ya mazungumzo yaliyopatanishwa na Qatar." Ni hawa wanaume wawili ambao walicheza dori kubwa katika mazungumzo ya yaliyofuatia.

2. Mazungumzo haya yalimalizika kwa Mkataba wa Doha wa tarehe 29 Februari 2020, jambo ambalo lilikuwa maarufu zaidi liliripotiwa na BBC News Arabic, ambayo ilisema, "Maafisa wa Amerika na Afghanistan walitangaza kuwa Amerika na washirika wake wa NATO wataondoa vikosi vyao kutoka Afghanistan ndani ya miezi kumi na nne, ikiwa Taliban itatimiza majukumu yao, chini ya makubaliano ambayo yalitiwa saini nchini Qatar jijini Doha leo. Tangazo hilo lilikuja katika taarifa ya pamoja ya Amerika na Afghanistan iliyotolewa jijini Kabul. Rais Donald Trump alisema ilikuwa "safari ndefu na ngumu" nchini Afghanistan. "Ni wakati sasa baada ya miaka hii yote kurudisha watu wetu nyumbani," alisema." BBC iliongeza, "Zaidi ya wanajeshi 2,400 wa Amerika waliuawa wakati wa mzozo huo."

3. Baada ya Makubaliano ya Doha, taarifa na mikutano ilikola kasi, licha ya kuendelea kwa mapigano, kwa viwango vya juu na vya chini.

CNN iliripoti mnamo 14 Aprili 2021 kwamba Joe Biden alitangaza, “Mimi sasa ni rais wa nne wa Amerika kusimamia uwepo wa vikosi vya Amerika nchini Afghanistan. Wawili wa chama cha Republican. Wawili wa chama cha Democtrats, aliendelea. "Sitapokeza jukumu hili kwa rais wa tano… Ni wakati sasa wa kumaliza vita virefu kabisa vya Amerika."

Biden kisha alitoa hotuba, ikifuatiwa na mkutano na waandishi wa habari uliopeperushwa kwenye runinga za Amerika na za kimataifa, mnamo 8 Julai 2021, akisema, "Tunavimaliza vita virefu kabisa vya Amerika ... Tulikwenda kwa sababu mbili: moja, kumleta Osama bin Laden... Sababu ya pili ilikuwa kuondoa al Qaeda… Tulitimiza malengo yote hayo - kwisha.” Alisema pia kwamba, "Misheni yetu ya kijeshi nchini Afghanistan itahitimika mnamo 31 Agosti." Aliongeza, "Hatukwenda Afghanistan kujenga taifa. Na ni haki na jukumu la watu wa Afghanistan peke yao kuamua mustakbali wao na jinsi wanavyotaka kuendesha nchi yao." Biden pia alisema, "Na tunahitaji pia kuzingatia kuongeza nguvu msingi za Amerika kufikia mashindano ya kimkakati na China…. Tunapaswa kuishinda COVID-19… Tunahitaji kuanzisha desturi za kimataifa za mtandao ... Na tutakuwa imara zaidi…. endapo tutapigana vita vya miaka 20 ijayo, sio miaka 20 iliyopita.”

Katibu wa Wanahabari wa Ikulu ya White House ya Amerika, Jen Psaki alisema kinaga ubaga, "hatutakuwa na wasaa "Misheni Imekamilishwa" katika suala hili. Ni vita vya miaka 20 ambavyo havijashindwa kijeshi." (Anatolia Arabic 8 Julai 2021), ikimaanisha kwamba Amerika haikupata ushindi nchini Afghanistan, licha ya miaka 20 ya kujaribu. Mnamo 2 Julai 2021, Amerika ilihamisha kambi yake muhimu zaidi na kubwa zaidi, Bagram, baada ya kufunga kambi nyenginezo hapo awali, ikimaliza kihakika vita vyake vya msalaba kabla ya tarehe rasmi iliyotangazwa na Rais Biden wa Amerika hapo awali, 11 Septemba, na kabla ya tarehe ya pili aliyoiweka, 31 Agosti.

Wakati huo, harakati ya Taliban ilipanua mashambulizi yake ya kijeshi na wilaya zikaanza kuanguka kaskazini, kusini, magharibi na kisha katikati. Kasi ya udhibiti wa harakati ya Taliban juu ya ardhi nyingi za Afghanistan ikawa isio na kifani, haswa kwenye mipaka ya nchi jirani, na pia kukamata kwao vivuko na nchi jirani. Shahabuddin Delawar, mwanachama wa timu ya mazungumzo ya Taliban jijini Moscow, alisema mnamo 9 Julai 2021, "asilimia 85 ya eneo la Afghanistan limeingia chini ya udhibiti (wa Taliban)," huku msemaji wa vikosi vya usalama vya Afghanistan, Ajmal Omar Shinwari, akikataa vikali hili, akisema: “Hii sio kweli. Mapigano yanaendelea katika maeneo mengi." (Agence France-Presse Arabic, 11 Julai 2021). Lakini, ujumbe wa Taliban uliahidi, "kutoingilia kati nchi jirani na nchi za kirafiki"… Yeye (Delawar) alisema kuwa ziara yake jijini Moscow inakusudia kutoa habari zote kuhusu kile alichokiita "Imarati ya Kiislamu." Aliongeza kuwa Taliban haitaruhusu upanuzi wa ISIS nchini Afghanistan na akasisitiza kuwa harakati hiyo itapambana nayo. Ujumbe huo pia ulithibitisha kwamba harakati hiyo inafanya mazungumzo na wawakilishi wa kijamii kufafanua muundo jumla wa dola na kwamba kazi hii inakaribia kukamilika… na kwamba harakati hiyo hailengi kunyakua mamlaka kikamilifu." (Al-Jazeera Arabic 9 Julai 2021).

4- Kisha ikatangazwa mnamo 17 Julai 2021, kwamba, "Pande hizo mbili za mzozo nchini Afghanistan zilikubaliana leo, Jumamosi, jijini Doha, kuunda kamati yenye wajumbe kumi na nne, kwa njia ya usawa, kujadili ajenda ya mazungumzo, ambayo yatajadili mambo ambayo yangali hayajatatuliwa. Mwandishi wa Al-Jazeera alinukuu chanzo katika mazungumzo ya Afghanistan jijini Doha, akisema kwamba kikao cha ufunguzi wa mazungumzo kilimalizika katika mazingira chanya. Raundi mpya ya mazungumzo kati ya serikali ya Afghanistan na harakati ya Taliban imezinduliwa leo katika mji mkuu wa Qatar, Doha na raundi hii inajadili mambo na maswala yaliyoelezewa kuwa ya muhimu. Abdullah Abdullah, Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Upatanishi wa Kitaifa la Afghanistan na mkuu wa ujumbe wa serikali, alisema kuwa kufanikiwa kwa amani nchini kunahitaji mnyumbuko kwa pande zote mbili, na kuongeza kuwa uwanja sasa mzuri kwa amani. Kwa upande wake, mkuu wa afisi ya kidiplomasia ya Taliban jijini Doha, Mullah Abdul Ghani Baradar, alisema kuwa watafanya kila wawezalo kufikia matokeo mazuri katika mazungumzo ya amani ya Afghanistan ambayo yameanza leo jijini Doha." (Chanzo: Al-Jazeera Arabic na Mashirika).

5. Kisha kamati ikakamilisha kazi yake leo, 18 Julai 2021, na taarifa ya pamoja ambayo ilitolewa kuhusu mkutano huo. Iliarifiwa kuwa, "Mwandishi wa Al-Jazeera jijini Doha alisema kuwa wajumbe wa serikali ya Afghanistan na harakati ya Taliban walifikia makubaliano juu ya taarifa ya mwisho ya pamoja ya mazungumzo yao yanayoendelea, jijini Doha na upatanishi wa Qatar, kufanya mkutano mwingine hivi karibuni kwa mkondo wa Doha. Pande hizo mbili zilikubaliana kuharakisha mazungumzo ili kupata suluhu ya haki kwa mzozo ambao umekuwa ukiendelea nchini kwa miongo kadhaa. Taarifa ya pamoja ya ujumbe wa serikali ya Afghanistan na Taliban iliainisha makubaliano ya kuharakisha mazungumzo ili kufikia suluhisho la haki, wakijitolea kufanywa kwa kiwango cha juu hadi suluhu ifikiwe. Kwa hivyo, ilimaliza raundi ya pili ya mazungumzo ya amani ya Afghanistan, ambayo yanalenga kufikia suluhu ya kisiasa ambayo inapelekea katika amani nchini, baada ya miongo kadhaa ya vita. Chanzo kimoja katika ujumbe wa Taliban kilisema kwamba harakati hiyo iliwasilisha pendekezo ambalo linajumuisha hatua za kujenga imani kati yake na serikali, kupitia kuwaachilia huru wafungwa pande zote mbili na kutangaza usitishaji wa mapigano katika kipindi cha Idd al-Adha ....” (Chanzo : Al Jazeera na mashirika.)

6- Inafaa kutaja msimamo wa dola mashuhuri ambazo Amerika huzitumia kwa uchangamfu katika mazungumzo na Taliban nchini Afghanistan:

a. Pakistan: Pakistan ndio iliyoishinikiza Taliban kufanya mazungumzo na Amerika mnamo 2018. Zalmay Khalilzad aliishukuru Pakistan kwa kuwezesha safari ya Taliban kwa ajili ya mazungumzo jijini Doha, huku Waziri wa Ulinzi wa Amerika, Lloyd James Austin III, katika mazungumzo ya simu mnamo 21 Machi 2021 na Mkuu wa Jeshi la Pakistan, Jenerali Bajwa, "alitoa shukrani kwa kuendelea kwa Islamabad kuunga mkono mchakato wa amani wa Afghanistan." (Mkuu wa Pentagon Asifu dori ya Pakistan katika Mchakato wa Amani wa Afghanistan, Jarida la Al-Fajr, Machi 23, 2021). Maafisa wakuu wa jeshi na viongozi wa kisiasa nchini Pakistan wamecheza dori kubwa katika mkakati wa Amerika kwa Afghanistan.

Kwa hivyo, dori ya Pakistan ni dori kubwa, sasa na kihistoria. Harakati ya Taliban ya Afghanistan ina asili ya Pakistan, kiasi ya kuwa ISI ya Pakistan na mashirika mengine ya kijasusi yana ushawishi wao nchini Afghanistan, huku wakiwa na mawasiliano na wanaume wao ndani ya Taliban. Hivyo basi, Amerika inategemea sana dori ya Pakistan.

b- Uturuki: Kama ilivyofanya nchini Syria na Libya, Uturuki inaelekea Afghanistan, ili kusaidia malengo ya sera za kigeni za Amerika. Wakati wa mkutano wa kimataifa katika hoteli ya kitalii ya Uturuki ya Antalya, Waziri wa Mambo ya nje wa Uturuki, Mevlut Cavusoglu, alipendekeza kuendeshwa na kulindwa kwa Uwanja wa Ndege wa Kabul na Uturuki ... Washington ilikubali kujitolea kwa Ankara kucheza dori muhimu katika kuulinda Uwanja wa Ndege wa Kabul, kufuatia mkutano wa Biden na Erdogan jijini Brussels mwezi uliopita. Amerika inataka Uturuki kutekeleza jukumu la ulinzi katika uwanja huo wa ndege, huku ikiwa bado inadumisha wanajeshi wake takriban 500 karibu na uwanja huo wa ndege wa kimataifa. Katika hotuba yake ya tarehe 8 Julai 2021, Biden aliashiria hilo, akisema, "tunashirikiana kwa karibu na washirika wetu wa kimataifa ili kuendelea kuulinda uwanja wa ndege wa kimataifa jijini Kabul." Erdogan alisema, "Tumeamua pamoja na Amerika na NATO mipango ya misheni ya mustakbali na kile tunachokikubali na kile tusichokikubali. Tuliibua suala hili wakati wa mikutano ya NATO, wakati wa mkutano wangu na Biden na wakati wa majadiliano kati ya wajumbe wetu. Tutatekeleza operesheni hii nchini Afghanistan kwa njia bora zaidi.” (Al Jazeera Arabic, 9 Julai 2021). Iliripotiwa mnamo 2 Julai 2021, kuhusu Msemaji wa Rais wa Uturuki, Ibrahim Kalin, "Uturuki itaendelea kulinda uwanja wa ndege wa Kabul hata baada ya wanajeshi wa NATO kuondoka Afghanistan msimu huu wa kiangazi, (Al-Awsat, 3 Julai 2021), huku harakati ya Taliban ikikataa uwepo wa Uturuki. Taliban ilitangaza katika taarifa moja, "Kukataa kwake kuviweka vikosi vya Uturuki nchini Afghanistan baada ya kuondolewa kwa vikosi vya kimataifa vinavyoongozwa na Amerika nchini na kusisitiza kuwa uamuzi kama huo ni wa kulaaniwa. Uamuzi huo wa uongozi wa Uturuki umeshauriwa vibaya, ni ukiukaji wa ubwana wetu na heshima ya eneo na dhidi ya maslahi yetu ya kitaifa… Na tunawasihi vikali maafisa wa Uturuki kubadili maamuzi yao kwa sababu ni mabaya kwa nchi zote mbili." (Al Jazeera, 13 Julai 2021)

c. Asia ya Kati: Amerika imekuwa ikiongea na viongozi katika Asia ya Kati juu ya kuweka upya baadhi ya vikosi vyake huko. Jarida la 'The New York Times' liliripoti kwamba maafisa wa Amerika wamekuwa wakiwasiliana na mamlaka za Kazakh, Uzbek na Tajik kuhusu uwezekano wa utumiaji wa kambi katika eneo hilo. Katibu wa Waziri wa Kigeni wa Amerika, Anthony Blinken, alisema katika msururu wa nukuu za tweets kwamba alizungumza mnamo Aprili 22 na mawaziri wa kigeni wa Uzbekistan na Kazakhstan juu ya utumiaji wa kambi za kijeshi wa Amerika na vikosi vyengine vya NATO. Jarida hilo la 'The New York Times' lilisema kwamba, "Droni, mabomu ya masafa marefu na mitandao ya kijasusi itatumiwa na Amerika na washirika wa Kimagharibi katika juhudi za kuzuia Afghanistan kujitokeza tena kama kambi ya kigaidi." (Jarida la 'The New York Times' 27 Aprili 2021)

7- Kwa kuzingatia hayo yaliyotajwa juu, ni wazi kuwa:

a- Mazungumzo yanayoendelea hayatapelekea kuondolewa kwa Amerika kutoka Afghanistan, lakini badala yake yatapelekea katika uhadaifu, kiasi ya kuwa Amerika inatoka kwa mlango wa mbele, na kuingia kupitia mlango wa nyuma, ambao unalindwa na vibaraka na wafuasi nchini Pakistan, Uturuki na Iran na wale wanaoduru pamoja nao miongoni mwa vibaraka wa Amerika ndani ya Afghanistan yenyewe, huku dola hizi zikicheza dori muhimu kwa ajili ya kudumisha ushawishi wa Amerika nchini Afghanistan…

b - Ama Qatar, inaandaa mazingira ya mazungumzo kwa malengo mawili: la kwanza, ni kwa ajili ya kubadilishana na Amerika kuondoa kizuizi cha Saudi au "kuzingirwa" dhidi yake, na hii ndio imekuwa hali ... haswa baada ya Makubaliano ya Doha kuhitimishwa mnamo 29 Februari, 2020 wakati wa utawala wa Trump ... na lengo la pili ni kwamba Qatar, Waingereza wakiwa nyuma yao, wameanza kutumia mawasiliano yao na Taliban kuiaibisha Amerika. Hii ni kutoka kwa upande wa kuingilia kwa makusudi, kwani wanatoa msaada wa kifedha kwa harakati ya Taliban na kupeana afisi ya kidiplomasia pamoja na jukwaa la vyombo vya habari kwao, kiasi ya kuwa Amerika baadaye ihitaji dori ya Qatar kuwezesha mawasiliano yake na harakati ya Taliban... Na hivi ndivyo Waingereza wanavyojiweka kwenye picha. Na Waingereza hutumia hii kutumikia maslahi yao nchini Qatar na Ghuba, wakitumia fursa ya haja ya Amerika ya dori ya Qatar katika kuwezesha mawasiliano na Taliban ...

C - Kuingia kwa Taliban katika mazungumzo na Amerika na vibaraka wake katika serikali ya Afghanistan ilikuwa ni kosa kubwa sana ... Tunamwomba Mwenyezi Mungu (swt), Mwenye uwezo na nguvu, kuwalinda Waislamu nchini Afghanistan kutokana na uovu wao, kwani makafiri wakoloni wanajadili tu kufanikisha maslahi yao, kwa sababu ya dhurufu zinazowalazimisha. Yule anayechunguza dhurufu hizi kwa makini zinazoilazimisha Amerika sasa atazione kuwa dhahiri. Kwa hivyo, kwa kila mwenye akili, husikiza na kuzingatia:

Kwanza: Kuibuka kwa China kama nguvu ya kijeshi na kiuchumi katika karne hii kunatishia maslahi ya Amerika ... Mwelekeo mpya wa Amerika kwake umekuwa kipaumbele. Taarifa za maafisa wa Amerika zinathibitisha kile tulichokitaja hapo awali juu ya hotuba ya Biden ya tarehe 8 Julai 2021, ambapo Biden alisema, "Na tunahitaji pia kuzingatia kuongeza nguvu za kimsingi za Amerika ili kukidhi ushindani wa kimkakati na China na mataifa mengine ambazo kihakika ndizo zitakazo amua – kuamua mustakbali wetu.”

Pili: Hasara zilizopatikana na Amerika nchini Afghanistan wakati wa uvamizi wake wa Afghanistan. Kama tulivyotaja hapo juu, ripoti ya BBC ya tarehe 29 Februari 2020 iliongeza, "Zaidi ya wanajeshi 2,400 wa Amerika wameuawa wakati wa mzozo."

Yote hii yanaashira kwamba Amerika ilikuwa inaondoka Afghanistan huku ikikunja mkia wake katikati ya miguu yake, bila ya kuondoka kupitia mazungumzo ambayo yanaipa ushawishi ambao haingeweza kuupata kupitia vita!

d- Tunatambua kuwa kuna ndugu wakweli na wenye ikhlasi ndani ya Taliban, kwa hivyo ni kwao ndio tunajielekeza sasa:

- Kwamba wasahihishe mambo kupitia kumaliza mazungumzo haya, ili wasiiwezeshe Amerika kufikia kile ambacho haingeweza kukifikia kupitia vita ...

- Na kwamba wawe na yakini kuwa suala kuu kwa Waislamu ni kurudishwa kwa Khilafah baada ya kutoweka kwa muda mrefu, kwani ni Faradhi iliyoamrishwa na Mwenyezi Mungu (swt) na ni utiifu kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) ...

- Na kwamba wajue kuwa kushiriki katika utawala wa mchanganyiko wa Uislamu na usekula haukubaliki kwa Mwenyezi Mungu (swt), kwa kuwa Mwenyezi-Mungu na Mwenye nguvu Muweza wa yote hakubali chochote isipokuwa kilicho kizuri …

Hii ndio haki kwani Mwenyezi Mungu (swt) asema,

[فَمَاذَا بَعْدَ الْحَقِّ إِلَّا الضَّلَالُ]

“Na kipo kitu gani baada ya haki, isipokuwa upotovu tu?” [TMQ Surah Yunus 10:32]. Na kufuata Haki pekee ndiko kutakakoiokoa Taliban, nchi, watu wake na Waislamu wote ... Hivi ndivyo Hizb ut Tahrir anavyokushaurini sasa, kama vile tulivyokushaurini mwanzoni mwa utawala wenu kutangaza Khilafah. Lakini, mlikataa na kisha mkajua kuwa mumekosea kwa kukataa huko, kama ilivyosemwa na Mullah Omar, Mwenyezi Mungu (swt) amrehemu, katika moja ya vikao vyake, lakini wakati huo ilikuwa ishachelewa ... Na sisi hapa tena tunarudia ushauri ule ule, hivyo basi je sasa kuna majibu chanya?

[يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اسْتَجِيبُوا لِلَّهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُمْ لِمَا يُحْيِيكُمْ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّهَ يَحُولُ بَيْنَ الْمَرْءِ وَقَلْبِهِ وَأَنَّهُ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ]

“Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.” [TMQ Surah Al-Anfal 8:24]

09 Dhul Hijjah 1442 H

19 Julai 2021 M

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu