Alhamisi, 09 Shawwal 1445 | 2024/04/18
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Siri ya Mapenzi, Utulivu na Heshima ndani ya Maisha ya Ndoa

Moja kati ya mahusiano adhimu ambayo Mwenyezi Mungu (swt) amewawekea wanadamu ni mahusiano kati ya mwanamume na mwanamke. Mahusiano haya ndio asili ya mahusiano yote yanayounda familia. Hivyo basi ni muhimu yaweko katika hali nzuri yenye kupelekea kufaulu. Mwenyezi Mungu (stw) asema:

هُوَ الَّذِي خَلَقَكُمْ مِنْ نَفْسٍ وَاحِدَةٍ وَجَعَلَ مِنْهَا زَوْجَهَا لِيَسْكُنَ إِلَيْهَا﴿

“Yeye ndiye aliye kuumbeni katika nafsi moja; katika hiyo hiyo akamfanya mwenzi wake, ili akae naye kwa utulivu.”  [7:189]

Mwenyezi Mungu (swt) ameweka muongozo kwa mambo yote ya wanadamu, ili watu waweze kuondokana na dhiki na kupata njia iliyo nyooka. Wataweza kufaulu au kufeli katika dunia na watazawadiwa au kuadhibiwa huko akhera kwa mujibu wa kujifunga kwao na muongozo huo. Moja ya sababu ya kwa nini familia ya Kiislamu inafaulu ni kwa kuweko na muundo makini ambapo kila mwanachama wa familia anajua dori yake. Jambo zuri zaidi kuhusiana na mahusiano ya kijamii katika Uislamu ni kwamba mtu anatenda kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (swt), ima ni mahusiano baina ya mume na mke, wazazi na watoto au mahusiano ya kifamilia. Kuyatekeleza kwa mujibu wa Maamrisho ya Mwenyezi Mungu (swt) ni jukumu muhimu la Kiislamu na ambalo litazalisha mapenzi, utulivu na heshima ndani ya ndoa na muundo wa familia.

Mtume (saw) alikuwa na mahusiano ya karibu mno na wake zake na familia yake. Mwenyezi Mungu (swt) asema:

لَقَدْ كَانَ لَكُمْ فِي رَسُولِ اللَّهِ أُسْوَةٌ حَسَنَةٌ لِمَنْ كَانَ يَرْجُو اللَّهَ وَالْيَوْمَ الْآخِرَ وَذَكَرَ اللَّهَ كَثِيرً﴿

“Hakika nyinyi mnayo ruwaza njema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa anaye mtaraji Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, na akamkumbuka Mwenyezi Mungu sana.” [33:21]

Ibn Maja amesimulia kwamba Mtume (saw) alisema: خَيْرُكُمْ خَيْرُكُمْ لأَهْلِهِ وَأَنَا خَيْرُكُمْ لأَهْلِي»» “Walio bora miongoni mwenu ni wale walio bora kwa wake zao, na Mimi ni mbora kwenu kwa wake zangu.”

Katika ndoa za Mtume (saw) kulikuweko na mapenzi, utulivu na heshima. Mtume (saw) alikuwa mwema kwa wake zake na sio dikteta, kwani uadilifu ni jukumu muhimu la mwanamume kwa mkewe. Alikuwa na mahusiano mema nao, alicheza nao, aliwafanyia dhihaka, aliwasaidia katika kazi zao za nyumbani alipokuwa na nafasi na kuwafunza masomo. Imesimuliwa na al Bukhari “Kila mara alijiunga nao katika kazi za nyumbani na wakati mwingine akishona nguo zake, viatu vyake na kufagia sakafu. Alikuwa akikama, akiwafunga na kuwalisha wanyama wake na kufanya kazi za nyumbani.” Mtume (saw) alikuwa ngao na mlinzi wa wake zake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu (swt):

الرِّجَالُ قَوَّامُونَ عَلَى النِّسَاءِ﴿  

“Wanaume ni ngao na walinzi wa wanawake.” [4:34]

Fauka ya hayo, Mtume (saw) alisisitiza usimamizi mwema na uliojaa makini kwa watoto na wazee. Yeye (saw) alisema: «لَيْسَ مِنَّا مَنْ لَمْ يَرْحَمْ صَغِيرَنَا وَيَعْرِفْ شَرَفَ كَبِيرِنَا»“Yeyote asiyewahurumia watoto wala kuwaheshimu wazee, sio katika sisi.” (Abu Dawood, Al-Tirmidhi) Na asema Mwenyezi Mungu (swt):

وَقَضَى رَبُّكَ أَلاَّ تَعْبُدُواْ إِلاَّ إِيَّاهُ وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا إِمَّا يَبْلُغَنَّ عِندَكَ الْكِبَرَ أَحَدُهُمَا أَوْ كِلاَهُمَا فَلاَ تَقُل لَّهُمَآ أُفٍّ وَلاَ تَنْهَرْهُمَا وَقُل لَّهُمَا قَوْلاً كَرِيمًا * وَاخْفِضْ لَهُمَا جَنَاحَ الذُّلِّ مِنَ الرَّحْمَةِ وَقُل رَّبِّ ارْحَمْهُمَا كَمَا رَبَّيَانِي صَغِيرًا﴿

“Na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata: Ah! Wala usiwakemee. Na sema nao kwa msemo wa hishima. Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea huruma. Na useme: Mola wangu Mlezi! Warehemu kama walivyo nilea utotoni.” [17:23-24]

Sifa kuu ya mwanamke ambaye mwanamume atapata furaha na amani ni Imani yake. Mtume (saw) alisema:«تُنْكَحُ الْمَرْأَةُ لأَرْبَعٍ لِمَالِهَا وَلِحَسَبِهَا وَلِجَمَالِهَا وَلِدِينِهَا فَاظْفَرْ بِذَاتِ الدِّينِ تَرِبَتْ يَدَاكَ»“Mwanamke anaolewa kwa moja ya sababu nne: utajiri wake, cheo chake, uzuri wake na kujifunga kwake na dini. Basi oa mwanamke mwenye dini, au kinyume chake utafeli.” (Saheeh Al-Bukhari)

Mwanamke mchamungu anaona moja ya majukumu yake makuu ndani ya ndoa ni kumtwii na kumfurahisha mumewe kwa kuwa ni jukumu aliloamrishwa na Mwenyezi Mungu (swt). Haimaanishi kattu kwamba mwanamke asiwe na maoni yake na asijadiliane na mumewe au kutoa ushauri juu ya masuala. Bali inamaanisha kuwa lazima amkubali mumewe kama mtoa maamuzi wa nyumba na kujitahidi kuweza kufaulisha hilo. Jukumu hilo halimdunishi mwanamke mbele ya mwanamume, lakini ni jukumu ambalo ndani yake anapata malipo kutoka kwa Mwenyezi Mungu kama anavyopata malipo mwanamume anapokuwa mwema na kumtendea wema mkewe na kumpa malezi bora kwa kadri ya uwezo wake. Mtume (saw) alisema: ‏«إذا باتت المرأة هاجرة فراش زوجها لعنتها الملائكة حتى تصبح»“Lau mwanamke atakuwa kando na kitanda cha mumewe usiku mzima basi Malaika walamlaani mpaka atakaporudi.” Na yeye (saw) alimuuliza mwanamke:

«أَذَاتُ بَعْلٍ أَنْتِ؟» قُلْتُ: نَعَمْ، قَالَ: «...فَإِنَّهُ جَنَّتُكِ وَنَارُكِ» “Una mume?” Akajibu: ‘Naam.’ Akasema: “... Basi yeye ni Pepo (Jannah) yako na Moto (Nar) wako.”

Ni ushahidi kutoka kwa mwenendo wa Mtume kwamba kuchunga haki na majukumu baina ya wanandoa hupelekea kufaulu kwa ndoa na natija yake ni amani katika maisha ya familia pamoja na ulezi wa watoto na uwiano wa mahusiano ya kifamilia. Hivyo basi, Mtume (saw) ndio kiigizo chema kwa Waislamu katika masuala yote maishani. Kwa sababu Mtume (saw) anaonyesha kwamba Taqwa na ikhlass ni katika kutekeleza sheria za Mwenyezi Mungu katika njia iliyo bora. Yeye (saw) anatuonyesha namna ya kuweza kujitoa mhanga na namna ya kutokuwa mtumwa wa matamanio na kiburi. Kwa hiyo, ikiwa Muislamu mwanamume au mwanamke atatekeleza majukumu yake katika ndoa na kumpa mwandani wake haki zake kiukamilifu, basi Mwenyezi Mungu atatia mapenzi, utulivu na heshima pande zote mbili katika ndoa yao.

لَيْسَ الْبِرَّ أَنْ تُوَلُّوا وُجُوهَكُمْ قِبَلَ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَلَٰكِنَّ الْبِرَّ مَنْ آمَنَ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَالْمَلَائِكَةِ وَالْكِتَابِ وَالنَّبِيِّينَ وَآتَى الْمَالَ عَلَىٰ حُبِّهِ ذَوِي الْقُرْبَىٰ وَالْيَتَامَىٰ وَالْمَسَاكِينَ وَابْنَ السَّبِيلِ وَالسَّائِلِينَ وَفِي الرِّقَابِ وَأَقَامَ الصَّلَاةَ وَآتَى الزَّكَاةَ وَالْمُوفُونَ بِعَهْدِهِمْ إِذَا عَاهَدُوا وَالصَّابِرِينَ فِي الْبَأْسَاءِ وَالضَّرَّاءِ وَحِينَ الْبَأْسِ أُولَٰئِكَ الَّذِينَ صَدَقُوا وَأُولَٰئِكَ هُمُ الْمُتَّقُونَ﴿

“Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi. Bali wema ni wa anaye muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii, na anawapa mali, kwa kupenda kwake, jamaa na mayatima na masikini na wasafiri, na waombao, na katika ukombozi wa watumwa na akawa anashika Sala, na akatoa Zaka, na wanao timiza ahadi yao wanapo ahidi, na wanao vumilia katika shida na dhara na wakati wa vita; hao ndio walio sadikisha, na hao ndio wajilindao.” [2: 177]

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Amanah Abed

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 12 Aprili 2020 06:52

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu