Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vichwa vya Habari 26/01/2021

Vichwa vya Habari:

• Taharuki za Ukraine Zapamba Moto

• Zaidi ya Mamilionea 100 Watoa Wito wa Ushuru wa Utajiri kwa Walio Matajiri Zaidi

• Kufeli kwa Jaribio la Bitcoin

Maelezo:

Taharuki za Ukraine Zapamba Moto

Katika mkutano mmoja na waandishi wa habari mnamo tarehe 19 Januari 2022, Rais wa Marekani Joe Biden alitabiri Urusi "itaingia" Ukraine na kuashiria "uvamizi mdogo" wa Moscow unaweza kusababisha nchi za Magharibi "kupigana kuhusu nini cha kufanya na kutofanya." Biden alionekana kuthibitisha kuwa kulikuwa na eneo la tashwishi kuhusiana na kizingiti halisi cha kichochezi cha jibu la Amerika. Mara tu baada ya mkutano huo, Ikulu ya White House ilitoa taarifa kufafanua maoni ya Biden, ikibainisha "kikosi chochote cha kijeshi cha Urusi kitakachovuka mpaka wa Ukraine" kitajumuisha "uvamizi mpya" na "kitakabiliwa na jibu la haraka, kali, na la pamoja." kutoka kwa Marekani na washirika wetu.” Matamshi hayo ya rais wa Marekani yalizua utata, huku maafisa wa Ukraine wakiripotiwa kumshutumu Biden kwa kumpa Rais wa Urusi Vladimir Putin "idhini [ya] kuingia Ukraine kwa raha zake." Maoni ya Biden yanaonyesha kuwa Magharibi itaushughulikia "uvamizi mdogo" kwa njia tofauti na uvamizi kamili.

Zaidi ya Mamilionea 100 Watoa Wito wa Ushuru wa Utajiri kwa Walio Matajiri Zaidi

Kundi la mamilionea na mabilionea zaidi ya 100 kutoka nchi tisa walichapisha barua ya wazi kwa viongozi wa serikali na wafanyabiashara, wakitaka ushuru wa kudumu wa kila mwaka wa utajiri kwa walio matajiri zaidi ili kusaidia kupunguza ukosefu wa usawa uliokithiri na kuongeza mapato kwa ongezeko endelevu, la muda mrefu katika huduma za umma kama vile huduma ya afya. Watia saini hawa ambao ni matajiri zaidi wanajiunga na kundi la sauti zinazoendelea kukua kote duniani zinazotaka watu matajiri zaidi kutozwa ushuru kwa kuzingatia rekodi ya mapato ya utajiri wa COVID-19 kileleni mwa jamii... mapato ambayo yamewafanya matajiri kumi kuongeza utajiri wao zaidi ya maradufu hadi kufikia dolari trilioni 1.5. Mabilionea 2,660 duniani sasa wana utajiri unaokaribia ukubwa sawa na uchumi wa China. Barua hiyo ilisema kwamba huku ulimwengu ukiwa umepitia mateso mengi katika miaka miwili iliyopita, matajiri hao wameona utajiri wao ukiongezeka wakati wa janga hilo na wachache sana - ikiwa wapo - wanalipa sehemu yao stahiki ya ushuru. Kikundi hicho kinazihimiza serikali “zitutoze kodi sisi, matajiri, na kututoza ushuru sasa.” Kikundi hicho kilichapisha barua yao wakati wa Ajenda ya wiki ya Jukwaa la Kiuchumi la Dunia la Davos, wakati ambapo washiriki wanatarajiwa kujadili changamoto na masuluhisho muhimu ya kimataifa. Kinasema isipokuwa wakuu wa nchi na serikali na Maafisa Wakuu Watendaji watambue "suluhisho rahisi na faafu linalowatazama usoni - kuwatoza ushuru matajiri," watu kote ulimwenguni "wataendelea kuona kile kinachoitwa kujitolea kwao kutatua matatizo ya ulimwengu kuwa si chochote ila usanii tu." Watia saini hao mashuhuri ni pamoja na mtayarishaji na mrithi wa filamu wa Kimarekani Abigail Disney, mjasiriamali wa asili ya Denmark-Iran Djaffar Shalchi, mjasiriamali wa Marekani Nick Hanauer, na mwanafunzi na mrithi wa Austria Marlene Engelhorn.

Kufeli kwa Jaribio la Bitcoin

Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) umeitaka El Salvador kubadili uamuzi wake wa kufanya zabuni halali ya Bitcoin. Mnamo Septemba, El Salvador ilikuwa nchi ya kwanza kuruhusu watumiaji kutumia mfumo wa sarafu ya kidijitali (cryptocurrency) katika shughuli zote, pamoja na dolari ya Marekani. El Salvador ilikuwa nchi ya kwanza kufanya majaribio ya sarafu hiyo ya kidijitali, ambayo imegeuka kuwa janga kwa taifa la Amerika ya Kati. Uamuzi huo ulisababisha maandamano makubwa kwa hofu kwamba ingeleta ukosefu wa utulivu na mfumko wa bei katika nchi hiyo maskini ya Amerika Kusini. Bitcoin imepoteza karibu nusu ya thamani yake tangu Novemba. Fedha za Bitcoin mithili ya sarafu zisizo na thamani ya dhati (fiat) hazina uegemezi wa kihakika na kwa hiyo ziko katika rehema ya walanguzi.

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu