Jumamosi, 11 Shawwal 1445 | 2024/04/20
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vichwa vya Habari 17/08/2022

Vichwa vya Habari:

  • Mwaka Mmoja Tangu Marekani Kushindwa Nchini Afghanistan
  • Vita Vikubwa vya Nyuklia Huenda Vikaua Watu Bilioni 5, Utafiti Waonyesha
  • China Yatangaza Mazoezi Mapya ya Kijeshi huku Wanasiasa zaidi wa Kiamerika Wakizuru Taiwan

Maelezo:

Mwaka Mmoja Tangu Marekani Kushindwa Nchini Afghanistan

Jumatatu tarehe 15 Agosti 2022 iliadhimisha mwaka mmoja tangu Taliban waingie Kabul na serikali ya iliyokufa ya Afghanistan iliyokuwa ikiungwa mkono na Marekani kuanguka rasmi. Kumekuwa na vurugu dogo sana nchini humo tangu wanajeshi wa Marekani kuondoka, lakini Waafghani sasa wanakabiliwa na mgogoro mbaya sana wa kibinadamu ambao unazidishwa na vikwazo vya Marekani na kunyakua kwa Washington fedha za benki kuu ya Afghanistan. Jarida la Wall Street Journal liliripoti Jumatatu kwamba utawala wa Biden umeamua kutoachilia dolari bilioni 7 katika akiba ya benki kuu ya Afghanistan ambazo zinazuiwa nchini Marekani huku mamilioni ya Waafghani wakikabiliwa na njaa. Utawala huo pia ulisimamisha mazungumzo na Taliban kuhusu fedha hizo. Umoja wa Mataifa umeonya kwamba asilimia 95 ya Waafghani hawapati chakula cha kutosha na kwamba karibu nusu ya watu wanakabiliwa na njaa kali. Afisa mmoja wa Umoja wa Mataifa alisema mnamo Machi kwamba hali hiyo inatishia "kizazi kizima cha Waafghan."

Vita Kamili vya Nyuklia Huenda Vikaua Watu Bilioni 5, Utafiti Waonyesha

Watu bilioni tano watakaokufa kutokana na vita vya kisasa vya nyuklia pamoja na athari ya baa la njaa la kiulimwengu -- inayochochewa na mashizi yanayozuia mwanga wa jua kwenye angahewa –  inawezekana kuzidi kwa mbali vifo vinavyosababishwa na milipuko hatari. Wanasayansi katika Chuo Kikuu cha Rutgers walichora athari za uwezekano wa matukio sita ya mzozo wa nyuklia. Vita kamili kati ya Marekani na Urusi, uwezekano wa kuwa hali mbaya zaidi, ingeangamiza zaidi ya nusu ya wanadamu, walisema katika utafiti uliochapishwa katika jarida la Nature Food.

Makadirio hayo yalitokana na mahesabu ya kiasi gani cha mashizi kingeingia angani kutokana na dhoruba za moto uliowashwa na kulipuka kwa silaha za nyuklia. Watafiti walitumia zana ya utabiri wa hali ya hewa inayoungwa mkono na Kituo cha Kitaifa cha Utafiti wa Anga, ambayo iliwaruhusu kukadiria uzalishaji wa mazao makuu kwa msingi wa nchi kwa nchi. Hata mzozo mdogo tu ungekuwa na matokeo mabaya kwa uzalishaji wa chakula duniani. Utafiti huo unajiri baada ya mzozo kati ya Marekani na Urusi kuibuka kufuatia uvamizi wa Urusi nchini Ukraine. Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Sergei Lavrov alionya mwezi Aprili kwamba kuna hatari "kubwa" ya vita vya nyuklia kuzuka.

China Yatangaza Mazoezi Mapya ya Kijeshi huku Wanasiasa zaidi wa Kiamerika Wakizuru Taiwan

China imetangaza mazoezi zaidi ya kijeshi pambizoni mwa Taiwan huku idadi kadhaa ya wanasiasa wa Marekani wakizuru taifa hilo la kisiwa. taharuki kati ya wawili hao imeongezeka hivi karibuni kufuatia ziara za wanasiasa wa Marekani. Mazoezi hayo yamekusudiwa kama "jibu madhubuti na kizuizi thabiti dhidi ya njama na uchokozi kati ya Amerika na Taiwan," wizara ya ulinzi ya China ilisema. Nancy Pelosi alikuwa Spika wa kwanza wa Bunge la Marekani kusafiri hadi kisiwa hicho katika kipindi cha miaka 25 aliposimama hapo mwanzoni mwa mwezi huu. Mazoezi ya hivi punde zaidi yalitangazwa wakati wajumbe wa bunge la Marekani la Congress walipozuru Taiwan. Bado haijafahamika wazi ni lini yatafanyika. Ujumbe huo ulijumuisha Seneta wa Democrat wa Massachusetts Ed Markey, Wawakilishi wa Democrat wa California John Garamendi na Alan Lowenthal, Mwakilishi wa Democrat wa Virginia Don Beyer, na Mjumbe wa Republican wa Samoa ya Marekani Aumua Amata. Kulingana na NBC News, walipangwa kukutana na viongozi wa Taiwan ili kuzungumza juu ya usalama, biashara, silsila za usambazaji na masuala mengine. Wizara ya Mambo ya Nje ya Taiwan imesema katika taarifa yake: "Katika wakati ambapo China inaendelea kuibua taharuki za kieneo, Bunge la Marekani la Congress kwa mara nyengine tena linaandaa ujumbe mzito kwenda Taiwan ili kuonyesha urafiki wake usio na hofu na kuonyesha uungaji mkono mkubwa wa Marekani kwa kisiwa hicho."

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu