Alhamisi, 18 Ramadan 1445 | 2024/03/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Silsila ya Maswali Yaliyowasilishwa kwa

Amiri wa Hizb ut Tahrir

Sheikh Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah Katika Ukurasa Wake wa Facebook

Jibu la Swali:

Kampuni katika Uislamu sio Mtu Bandia

Kwa: Abu Rashed

(Imetafsiriwa)

Swali:

Sheikh wetu mheshimiwa, Assalam alaikum wa rahmatullahi wa barkatuh. Ninaacha mikononi mwako baadhi ya maswali kwa matumaini kwamba yatajibiwa. Mwenyezi Mungu akulipe kwa niaba yetu na akujaalie ushindi na uwezo chini ya mikono yako. Yeye ni Mwenye kusikia na Mwenye kuitikia kila kitu.

1) Makampuni, viwanda na alama za biashara

Tunajua kwamba makampuni katika Uislamu lazima yawe na mwili ndani yao. Ikiwa kampuni imeanzishwa kwa madhumuni ya kuanzisha kiwanda kinachozalisha, kwa mfano, vifaa vya umeme au vya elektroniki, na kampuni hii na kiwanda chake kuwa alama ya biashara inayojulikana sokoni, basi hutokea kwamba wamiliki wa kampuni wanataka kuiuza:

a) Je, kuna kitu katika Uislamu kama "thamani ya soko la kampuni" mbali na suala la hisa katika urasilimali?

b) Je, alama ya biashara ina thamani ya kutathminiwa wakati kiwanda kinauzwa?

c) Je, alama ya biashara ni ya kiwanda au kampuni, yaani, ikiwa kampuni itabaki na kuuza kiwanda chake kimoja au laini ya uzalishaji kwa moja ya vifaa vyake, ni nini kinachozingatiwa katika kukadiria bei?

d) Katika tukio la kampuni kuvunja, nini kitatokea kwa alama ya biashara?

e) Kiwanda cha kampuni kina mauzo ya nje na uagizaji, na kinaweza kuwa na madeni kwa wasambazaji wa malighafi, kwa mfano, na ina pesa inayodaiwa na wafanyabiashara kwa masharti tofauti. Je, ni muhimu "kusifuri" madeni na mapokeo kabla ya kuuza, kwa kujua kwamba huu ni mchakato wa kuendelea wakati wote mradi kuna uzalishaji?

f) Vipi kuhusu wafanyikazi na mikataba yao na kampuni wakati wa kuuza kiwanda?

2) Makampuni ya huduma

Kuna kampuni ambazo uundaji wao hauhitaji mtaji mkubwa, kwani hutoa huduma, kwa mfano, kampuni ya programu, ambayo imejengwa juu ya fikra, kwa hivyo hutengeneza programu moja au zaidi au aplikesheni na kuiuza kwenye soko, na aplikesheni hii  (ambayo ni misimbo ya programu tu inayofanya kazi fulani) inakuwa ina dadi kubwa ya watumiaji. Kwa hivyo, kampuni hii inaweza kuwa na thamani kubwa ya soko ipasavyo. Wakati aplikesheni inauzwa kwa upande mwingine (kampuni nyingine), inauza wazo na laini za code zinazotokana nalo ili isiwe na haki ya kuitumia baada ya kuuza, kwa hiyo inazalisha lile lile (yaani wazo). Mfano wa hili ni aplikesheni ambayo huhesabu njia ya gari kutoka sehemu moja hadi nyingine na kuchagua barabara bora Zaidi na wakati wa kuwasili, nk. Je, uhalisia huu unashughulikiwaje katika Uislamu?

Jibu:

Walaikum Assalam wa Rahmatullahi wa Barkatuh

Kwanza kabisa, Mwenyezi Mungu akubariki kwa dua zako nzuri kwa ajili yetu, na tunakuombea kwa kila la kheri.

Kwanza: Kabla ya kujibu maswali yako mengi, naomba kubainisha kwamba makampuni katika Uislamu ni tofauti na makampuni ya mfumo wa kirasilimali, hivyo kampuni   kisheria ni (mkataba kati ya wawili au zaidi, ambao wanakubali kufanya biashara ya kifedha, kwa nia ya kupata faida). Kampuni katika Uislamu si shakhsiya bandia ambayo vitendo vinapatikana kutoka katika sifa hii, vinginevyo vitendo hivi vitakuwa batili kwa mujibu wa Shariah. Badala yake, ni mahususi ambamo meneja anahitajika, na tumefafanua jambo hili katika kitabu, Nidhamu ya Uchumi, tulipotafiti kampuni za hisa za pamoja na kutokuwa halali kwao, kwa hivyo tulisema:

"Kampuni ni mkataba juu ya utumiaji (tasaruf) wa mali. Hivyo, ongezeko la mali kwa kutumia kampuni ni ongezeko la umiliki. Kuongeza umiliki ni moja ya tasaruf inayoruhusiwa na Shariah. Utumiaji wote wa Kishariah ni utumiaji wa kimaneno ambao hutoka kwa mtu na sio kutoka kwa mali. Ongezeko la umiliki lazima litokee kwa yule anayeweza kutumia, yaani, kutoka kwa mtu na mali.

Vitendo vinavyotokana na kampuni hiyo katika hali ya utu wake bandia ni batili kwa mtazamo wa Shar’a. Hii ni kwa sababu utumiaji unapaswa kutoka kwa mtu wa kihakika na mtu huyu anapaswa awe mmoja wa wale walio na haki ya utumiaji…

Matendo yanakubaliwa tu katika Shar’a kutoka kwa mtu ambaye ana uwezo wa kutasarraf na ni mtu mzima na mwenye akili timamu, mwenye akili ya utambuzi. Kitendo chochote ambacho hakitokani na maana hii ni batili kwa mtazamo wa Shar’a. Kuikabidhi tasarruf kwa shakhsiya bandia ya shirika kwa hivyo hairuhusiwi, badala yake inaregeshwa kwa mwanadamu ambaye ana uwezo wa kutenda…] Mwisho wa kunukuu.

Kwa maana nyengine, biashara na shughuli za kampuni katika Uislamu hazitenganishwi na kampuni yenyewe na washirika, hivyo kampuni haiwezi kuwa ni kitu na shughuli zake na matendo yake yakawa ni kitu kingine. Lakini baadhi ya maswali uliyouliza yanaonesha kuwa yanaathiriwa na uhalisia wa kiutendaji wa makampuni ya nchi za Magharibi, ambapo baadhi ya shughuli zao zinaweza kuwa tofauti nazo, hivyo kampuni ina shakhsiya bandia iliyojitenga na viwanda vyake, kwa mfano...Hili ni jambo lisilofikirika katika kampuni kwa mujibu wa Sharia. Badala yake, kampuni katika Shar’a haiwezi kutenganishwa na washirika, hasa washirika wa mwili, na haitenganishwa na biashara na shughuli zake kwa sababu mkataba wa kampuni umejengewa juu ya na vitendo na shughuli hizi...

Pili, majibu ya maswali yako:

1- Kampuni katika Uislamu kwa jina lake na jina linalojulikana haliuzwi wala kununuliwa, bali inaweza kuvunjwa kwa makubaliano ya washirika kwa namna ya kisheria, na mali na faida zake hugawanywa miongoni mwa washirika kulingana na kiasi cha ushiriki wao, na kisha kampuni inakwisha, yaani, kuwepo kwake hukoma, si kwamba huuzwa kwa upande mwingine, na kampuni inabakia kwa jina lake na kwa uwezo wake, lakini badala yake inachukuliwa na wale ambao wamenunua! Kwa hivyo, kampuni haina thamani ya mali yenyewe, kwa sababu kampuni ni (mkataba kati ya wawili au zaidi, ambao wanakubali kutekeleza kitendo cha kifedha, kwa nia ya faida), yaani, kampuni katika Uislamu ni ushirikiano na usajili, na sio shakhsiya bandia iliyotenganishwa na wamiliki wake kama ilivyo katika baadhi ya sura zake katika mfumo wa kirasilimali…Ama kile kinachonunuliwa na kuuzwa, inawezekana katika sharia mali ya kampuni kuwa majengo, mitambo, eneo na ubora wa uzalishaji, na kadhalika, ambayo muuzaji na mnunuzi wanakubaliana ... Ikiwa uuzaji unafanywa, kampuni ya zamani na wamiliki wake wameisha na kuwa kampuni mpya na wamiliki wapya ..

2- Unachokiita "thamani ya soko ya kampuni" au kiwanda ikiwa inahusiana na kile kinachoruhusiwa katika Sharia, kama nembo ya biashara, alama ya biashara, sifa, wateja na mambo mengine ambayo yanafanya kiwanda au kampuni kuwa na thamani zaidi kuliko thamani ya mali ya kiwanda au kampuni. Katika hali hii, mambo haya yanaweza kuzingatiwa katika kutathmini kiwanda wakati wa kukiuza, au kutathmini kampuni wakati mmoja wa washirika anataka kuiacha ili kukadiria stahili zake... Lakini ikiwa ni kwa sababu ya mambo yasiyoruhusiwa, kama milki ya kifikra na mengineyo, haijuzu kuitazama katika tathmini iliyotajwa hapo juu.

3- Ikiwa kampuni ina nembo ya kibiashara au alama ya biashara ambayo inatabanni katika bidhaa za moja ya viwanda vyake, na haina jina la kampuni juu yake, lakini kiwanda tu, inaweza, ikiwa inataka kuuza kiwanda hicho, kuuza nembo ya biashara na alama ya biashara kulingana na kiwanda, lakini iwapo nembo ya biashara na alama ya biashara ina jina la kampuni inayouzwa, itakwisha kwa mauzo ya kampuni.

4- Alama ya biashara, kama tulivyotaja, inaonyesha huluki inayozalisha bidhaa hiyo, na thamani yake inatokana na ubora wa bidhaa na sifa inayopatikana kwa mzalishaji wa bidhaa sokoni, nk. Ikiwa kampuni inayozalisha bidhaa hiyo itavunjwa na uzalishaji ukaisha, alama ya biashara itabatilika kulingana na kuvunjwa kwa kampuni. Sio sawa kwa mtu yeyote kuigiza kwa ajili yake mwenyewe kwa sababu sio yake ... Lakini ikiwa mmoja wa washirika anataka kuondoka kwenye kampuni, thamani ya alama ya biashara inaweza kuzingatiwa wakati wa kutathmini mali ya kampuni, ili kumpa mshirika asiyekubali haki yake katika kampuni.

5- Kuhusu swali lako: Kiwanda chenye uhusiano na kampuni kina mauzo ya nje na uagizaji, na kinaweza kuwa na deni linalodaiwa na wasambazaji wa malighafi, kwa mfano, na kina pesa zinazodaiwa na wafanyibiashara kwa masharti tofauti. Je, ni lazima "kusifuri" madeni na mapokeo kabla ya kuuza, kwa kujua kwamba huu ni mchakato endelevu wakati wote kunapokuwa na uzalishaji?, kiwanda katika Uislamu si tofauti na kampuni, badala yake ni kazi yake au ni moja ya kazi zake, na inayodaiwa deni sio kiwanda kwa sababu kiwanda sio umbile la kipeke yake, bali ni kazi na shughuli za kimada tu. Mwenye kudaiwa na wengine na mwenye kuwadai wengine ni kampuni ambayo kiwanda kilikuwa ndio kazi yake au ilikuwa moja ya biashara yake. Kiwanda kikiuzwa basi kinachouzwa ni vifaa vya ujenzi, uzalishaji na vitu vilivyoambatanishwa, lakini haki zinazodaiwa na kampuni na haki za kampuni lazima zivunjwe na kampuni pamoja na mamlaka husika mbali na suala hilo la kuuza kiwanda, hivyo hairuhusiwi kwa mujibu wa Shar'a kukiuza kiwanda hicho pamoja na madeni na dhima zake, kama inavyotokea katika mfumo wa kiraslimali.

6- Kuhusiana na swali lako: Vipi kuhusu wafanyikazi na mikataba yao na kampuni wakati kiwanda kinauzwa?, mikataba ya hawa wanaolipwa mishahara iko kwenye kampuni kwa sababu kiwanda si chombo cha usimamizi, bali ni kazi ya kampuni au ni moja ya biashara yake. Ikiwa kampuni inauza kiwanda wanachofanyia kazi, basi kazi yao katika kiwanda inaisha wakati nafasi yao inapokwisha kwa uuzaji wa kiwanda. Hapa, kampuni inaweza kuwakabidhi kazi zingine katika maeneo mengine ya biashara ya kampuni huku ikidumisha mikataba yao ya uajiri hadi mwisho wake, na inaweza kuwalipa ujira wao kwa muda uliobaki wa uajiri bila kuwamiliki, na inaweza, kwa makubaliano nao, kusitisha mikataba yao nao ili mmiliki mpya wa kiwanda aanzishe mikataba mipya nao. Endapo ataona inafaa kwake kutokana na uzoefu wa hawa wanaolipwa mishahara... Yote hayo yameachiwa makubaliano ya wahusika... Hata hivyo, mikataba ya uajiri ya watumishi hawa wa kuajiriwa inabaki kuwa halali kwenye kampuni hadi kuisha kwa muda wao, kwani mikataba ya uajiri katika Uislamu ni ya lazima na lazima ibainishwe kwa muda maalum na inaisha mwisho wa kipindi hicho ikiwa haitafanywa upya.

7- Kuhusiana na swali lako kuhusu kampuni za programu na aplikesheni, programu na aplikesheni ni bidhaa ambazo zina faida, kwa hivyo inaruhusiwa kwa mujibu wa Shar'a kuziuza, yaani, inaruhusiwa kwa kampuni iliyotengeneza programu au aplikesheni kuuza kwa mhusika mwengine asili ya programu au aplikesheni ili kuipa taarifa na misimbo husika. Katika hali hii, kampuni ya kwanza iliyouza programu au aplikesheni hairuhusiwi kwa mujibu wa Shar'a kuendelea kutumia programu au aplikesheni hii maadamu imeiuza na asili yake, yaani iliuza wazo ambalo aplikesheni hiyo ilitegemea na kujitolea katika mkataba wa mauzo kutoitumia.

Natumai kwamba majibu haya yanatosheleza, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi na Mwenye hikima.

Ndugu Yenu,

Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

28 Rabi’ al-Awwal 1444 H

24/10/2022 M

Link ya jibu hili kutoka ukurasa wa Amiri wa Facebook.

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu