Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Hakuna Ukandamizaji Isipokuwa Humrudia Mkandamizaji!

Tukiwa tumekamilisha saum za mwezi wa Ramadhani na kuingiliwa na masiku ya kusherehekea Eid ul-Fitr hatuna budi ila kuwakumbuka ndugu zetu walio katika hali ya kusikitisha mno. Hali ambazo hazifai kuwafika Wanyama, Miti hata na Mawe licha Wanaadamu. Hali hii imekuwa ni kama kawaida kwa ndugu zetu wa Syria, Iraq, Yemen, Falastin na maeneo mengi ya Waislamu. Madhila yote haya yanayowapata Umma wa Kiislamu yana mkono wa mbepari anaochukuliya huu ulimwengu kuwa ni shamba lake- Mmarekani. Upande mwengine kuna baadhi ya watawala, wakuu wa kijeshi, wanasiasa na hata mashekhe katika biladi za Kiislamu wanaomsaidia Taghut huyu katika kufanikisha malengo yake hata kama itapelekea kumwaga damu tukufu za Waislamu wakiwa na matarajio na wao watapata japo makombo washibishe matumbo yao na watu wao wa karibu!

Amma hapa kwetu Kenya pia Mwezi wa Ramadhani umeingia na kuondoka ikiwa hali ya Waislamu ni yakusikitisha bila ya kuwa na mtetezi wa kuwasemea katika madhila hayo. Kuna walowakosa wapendwa wao wasijulikane wako wapi wala wasijue wakuwapelekea mashtaka yao licha ya kua waliwapoteza wanajulikana. Hii imekua ni siri iliowazi kuwa vyombo vya usalama wa nchi ndio wahusika wakuu katika kuwashika vijana kwa mamia na kuwapoteza kama ilivyonukuliwa katika ripoti zilizo tolewa na vyama vinavyotetea haki za kibinaadamu. Na kama ilivyo kiulimwengu ajenda hii inaendeshwa na Marekani kupitia kuzibururza ‘nchi rafiki’ katika ulimwengu wa tatu ikiwemo Kenya katika kuwadhalilisha maraia wake Waislamu ili wafikie malengo yao. Na vile vile serikali hizi zetu huwatumia viongozi wa Kiislamu wakiwemo wanasiasa, wahusika wakiusalama na haswa mashekhe kuhalalisha madhila haya. Wanauza akhera yao kwa chumo dogo la kidunia! Sisi twawakumbusha kuwa yoyote atakae simama na dhulma basi ajue yatamrudia hapa hapa duniani kwa hizaya na kesho akhera ni hesabu kali kutoka kwa Mwenyezi Mungu (swt).

Mfano mzuri wa haya ni matukio yaliyotokea hivi karibuni kushikwa kwa wabunge wa pande zote mbili- serikali na upinzani almaarufu ‘Pangani Six’ ambao walitiwa korokoroni bila mashtaka. Silaha ya utungaji sheria za kupambana na ugaidi ambazo zimepetishwa na Bunge kwa kushurutishwa na Marekani ili kupunguza kasi ya wito wa Uislamu ndizo zilizotumiwa kuwafunga wabunge wanane bila mashtaka chini ya sheria zilezile zinazochukiwa ambazo walizipitisha kwa kumtumikia Muamerika katika vita vyake vya ulimwengu dhidi ya Uislamu. Wabunge hawa waliamini kuwa wako salama kutokana na athari za vitendo vyao kwa kuungana na wakandamizaji lakini Mwenyezi Mungu (swt) asema:

 (وَسَكَنتُمْ فِي مَسَاكِنِ الَّذِينَ ظَلَمُوا أَنفُسَهُمْ وَتَبَيَّنَ لَكُمْ كَيْفَ فَعَلْنَا بِهِمْ وَضَرَبْنَا لَكُمُ الْأَمْثَالَ) "Na mkakaa katika maskani zile zile za walio zidhulumu nafsi zao. Na ikakudhihirikieni jinsi tulivyo watendea. Nasi tukakupigieni mifano mingi." [Ibrahim:45]

Ama kuhusu dhana ya uongo ya kuwa salama kwa kuwafanya wakandamizaji kuwa washirika, Mwenyezi Mungu (swt) anafichua:

(يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَتَّخِذُوا آبَاءَكُمْ وَإِخْوَانَكُمْ أَوْلِيَاءَ إِنِ اسْتَحَبُّوا الْكُفْرَ عَلَى الْإِيمَانِ ۚ وَمَن يَتَوَلَّهُم مِّنكُمْ فَأُولَٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ) "Enyi mlio amini! Msiwafanye baba zenu na ndugu zenu kuwa vipenzi vyenu ikiwa wanastahabu/wanapenda ukafiri kuliko Imani. Na katika nyinyi atakaye wafanya hao ndio vipenzi vyake, basi hao ndio madhaalimu." [At-Taubah:23]

Kwa katiba ile ile ya ukandamizaji na sheria walizoapa kwa Bwana wao kuzilinda na kuzitekeleza juu ya wajinga na wanyonge imekuwa ndio chanzo cha kujidhalilisha na kujikandamiza wenyewe. Sheria zile zile za kufungwa kabla kushtakiwa ambazo waliungana na mkandamizaji wa binadamu Amerika na washirika wake ili zitumike dhidi ya Waislamu zimetumika dhidi yao wenyewe, na haya yataendelea kwa njama zao zote walizozipangia Dini Tukufu ya Uislamu na Umma wake mtukufu. Hawatosazwa kutokana na kushikwa ovyo ili kujaza majela yatakayojengewa ‘Walio na Misimamo Mikali’ (Waislamu). Walio na macho watizame na walio na akili watafakari juu ya maneno ya Muumba, Mwenyezi Mungu (swt) anaposema:

(وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أنزَلَ اللّهُ فَأُوْلَـئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ) "Na wasio hukumu kwa yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio madhaalimu." [Al-Ma’idah:45]

Tunatoa wito kwa معاون لظالمين Wasaidizi na Washirika wa Wakandamizaji, kuwa watu waliojitwika sifa za Mwenyezi Mungu kimatamshi na kivitendo kwa kujiita wao ‘Watungaji Sheria’, na wale wanaotumika kama Sauti za Wakandamizaji (Waandishi wa habari, Wasemaji wa Serikali na Wasomi), wanaotumika kama Mikono ya Wakandamizaji (Wanajeshi, Magavana, Mawaziri na Washauri), na wanaotumikia kama Macho ya Wakandamizaji (Upelelezi, Wapelelezi, Mawakala, Wanaoripiti) kwamba wote waache kuwasaidia na kuandamana na Wakandamizaji , maanake Mwenyezi Mungu (swt) anaonya:

(وَلَا تَرْكَنُوا إِلَى الَّذِينَ ظَلَمُوا فَتَمَسَّكُمُ النَّارُ وَمَا لَكُم مِّن دُونِ اللَّهِ مِنْ أَوْلِيَاءَ ثُمَّ لَا تُنصَرُونَ) "Wala msiwategemee wanao dhulumu, usije ukakuguseni Moto. Wala nyinyi hamna walinzi badala ya Mwenyezi Mungu, wala tena hamtasaidiwa."[Hud:113]

…njia ambayo inapelekea katika udhalilishaji/hizaya duniani kama Seneta Billow Kerrow, Seneta Ali Bule na sasa Junet Muhammad wameshuhudia baada ya kushikwa kwa muda mfupi na kuwekwa kizuizini, na uwezo wa kukutana na mwisho kama wa Qaddafi na Saddam Hussein na familia zao licha ya miaka mingi ya kuihudumia Nidhamu ya Kikafiri, hatimaye ni mateso na adhabu ya milele kutoka kwa Mmoja (swt) aliyewapa uhai.

Sisi twawaita warudi wasimame na haki ya Uislamu, wafanyekazi na Umma mtukufu kwa kutoa kiakili, kijamii, kiuchumi, kisiasa na kiroho uwongofu utokao kwa Mwenyezi Mungu (swt) na mwenendo wa Mtume (saw) unaotokamana na Dini Tukufu ya Uislamu kwa wanadamu wote. Ili kuwakomboa wanadamu na dunia kutoka katika maangamivu ya makucha ya waasi waliokwenda kinyume na Bwana wao.
Imepokewa kutoka kwa Ibn Umar: Mtume Muhammad (saw) alisema:

«مَنْ أَعَانَ عَلَى خُصُومَةٍ بِظُلْمٍ - أَوْ يُعِينُ عَلَى ظُلْمٍ - لَمْ يَزَلْ فِي سَخَطِ اللَّهِ حَتَّى يَنْزِعَ»“Yeyote anayesaidia katika mzozo wowote kumdhulumu au kushirikiana na anayedhulumu ataendelea kukasirikiwa na Mwenyezi Mungu mpaka anapoangamia (kufa)” [Ibn Majah katika kitabu chake cha Al-Ahkam]

Mwisho hakuna mfumo utakao weza kusimama dhidi ya dhulma za mfumo huu wa kibepari unaongozwa na Marekani ila mfumo wa Uislamu utakao tawalishwa na Khilafah kwa njia ya Utume na kuwaokoa si tu Waislamu bali hata wasiokua Waislamu kutokana na unyanyasaji huu ambao haujawahi kuonekanwa katika tarehe ya Kibinadamu. Lakini haya yahitaji juhudi za pamoja kusimama na kupinga bila ya kunyamaza kwa ajili ya khofu. Hizb ut Tahrir kiulimwengu ina simama na kupinga kiwazi ubepari wa kiurasilimali bila ya kujali lawama ya mwenye kulaumu na vitisho vya wenye kutisha. Hii ni changamoto kwa kila mwenye kutaka mabadiliko ya kweli ili kuondoa dhulma hizi.

Twamalizia kwa kumuomba Mwenyezi Mungu (swt) atutakabalie amali zetu za Funga na Qiyam na kuwatakia Waislamu wote Eid ya fanaka na furaha. Wa Kullu ‘Aam Wa Antum Bi Kheir!

H. 1 Shawwal 1437
M. : Jumatano, 06 Julai 2016

Hizb-ut-Tahrir

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu