Jumamosi, 21 Muharram 1446 | 2024/07/27
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Kupigania Utukufu wa Kijeshi na Kiraia Kumeifikisha Pakistan kwenye Ukingo wa Maangamivu. Uokovu Wetu Pekee ni kwa Utukufu wa Shariah, kupitia Kusimamisha Khilafah kwa Njia ya Utume

(Imetafsiriwa)

Kwa muda wa wiki kadhaa zilizopita, siasa za Pakistan zimeshikiliwa na ubabe, uhasama, machafuko na ukosefu wa utulivu. Sababu ya mgogoro huu wa kisiasa ni mapigano ya kindani ya makundi ya wenye ushawishi kati ya majaji, majenerali na wanasiasa. Hakuna kundi lolote linalojali matatizo halisi ya watu. Makundi hayo yanapigania madaraka tu. Hakuna chochote ndani yake kwa ajili ya watu wa Pakistan. Wananchi wamezama kwenye shida kubwa za kiuchumi, na wamepigwa na ukataji tamaa mkubwa.

Katika mvutano wao wa madaraka, majaji, majenerali na wanasiasa wamezua mgawanyiko mkubwa wa kijamii. Waislamu wa kawaida waligeuka dhidi ya watoto wao wenyewe katika vikosi vya jeshi. Mali ziliharibiwa, matukufu yalikiukwa na damu takatifu ya Waislamu ilimwagika. Kugombana kwa jeshi dhidi ya raia kunawadhoofisha Waislamu tu. Ni kama vile vile vinavyoitwa ‘Vita dhidi ya Ugaidi,’ wakati Waislamu walipopigana na Waislamu ili kupata maslahi ya wakoloni wa Kimarekani kwenye mpaka na Afghanistan. Pakistan ilidhoofishwa mbele ya India, na hatimaye India ilinyakua ardhi za Kiislamu za Kashmir. Amesema Mwenyezi Mungu (swt):

[وَاَطِیْعُوا اللّٰهَ وَرَسُوْلَهٗ وَلَا تَنَازَعُوْا فَتَفْشَلُوْا وَتَذْهَبَ رِیْحُكُمْ]

“Na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msizozane mkaingiwa woga, na zikapotea nguvu zenu.” [Surah Al-Anfal 8:46].

Licha ya mvutano juu ya mamlaka kati yao wenyewe, majaji, majenerali na wanasiasa wanakubaliana kamilifu juu ya muundo wa kisekula wa serikali. Muundo huu umetekelezwa na kipote cha watawala wa Pakistan kwa zaidi ya miongo saba, ili kutumikia mfumo wa kilimwengu wa Marekani. Chini ya mfumo huu wa serikali ya kisekula, vikundi vya kijeshi pamoja na vya kiraia vimeendelea kutekeleza sera za kiuchumi za kibepari, zenye kuendelea kushusha thamani ya sarafu ya Pakistan. Kwa maagizo ya IMF ya kikoloni, watu wamekuwa chini ya umaskini, mfumko wa bei na kunyimwa. Hii ni huku utajiri wa wawekezaji wenye riba ukiendelea kuongezeka, huku mkusanyiko mkubwa wa rasilimali ukiwa mikononi mwa wachache. Makundi yote ya kijeshi na ya kiraia yalihakikisha kwamba Pakistan ilikuwa tegemeo kwa maslahi ya Marekani, huku Jeshi la Pakistani likitumiwa kama kikosi cha mamluki.

Makundi haya tawala ya wenye ushawishi pia yanakubali kwamba Uislamu hauna nafasi katika utawala, uchumi, mahakama na sera za kigeni. Wanatumia tu jina la Uislamu kupata uungwaji mkono na watu wanaopenda Uislamu wa Pakistan. Hata hivyo, wamejitolea kwa maamuzi na sheria za kibinadamu daima wakiwa na utukufu juu ya Shariah iliyoteremshwa na Mwenyezi Mungu (swt). Makundi yanayotawala yanahakikisha kwamba Uislamu kamwe sio msingi wa siasa na dola. Wanafanya hivyo wakiwa na matumaini ya kupata idhini ya Magharibi, kutambuliwa na kusifiwa, pamoja na uungwaji mkono thabiti wa Marekani kwa uamuzi wao.

Mvutano kati ya makundi yanayotawala umekuwa ukiendelea sasa kwa miaka 76 iliyopita. Wakati mwingine hufifia, na wakati mwingine huibuka kama mgogoro mkali wa kisiasa. Wakati fulani kunakuwa na mzozo kati ya uongozi wa kiraia na kijeshi, na wakati mwingine kunakuwa na mzozo ndani ya jeshi wenyewe juu ya wadhifa wa mkuu wa jeshi. Mizozo inaendelea kwa sababu Demokrasia yenyewe inahakikisha mivutano yenye madhara juu ya madaraka. Mamlaka ya kutunga sheria ya kibinadamu katika Demokrasia huruhusu makundi yenye ulafi, yenye nguvu kutunga sheria ili kuhakikisha maslahi yao, kusalia madarakani na kudhibiti rasilimali za serikali. Maadamu Demokrasia itabakia, mizozo ya kisiasa juu ya madaraka itaendelea.

Enyi Waislamu wa Pakistan! Mafanikio ya taasisi ya jeshi na washirika wake wa kisiasa, PDM sasa au PTI kabla yake, na washirika wake katika mahakama hayatatuletea afueni yoyote. Pande zote mbili zinataka kulazimisha mfumo mmoja wa kidemokrasia wa kibepari, ambao ndio chanzo cha matatizo yetu. Mvutano juu ya "ukuu wa kijeshi na kiraia" ni kupoteza juhudi zetu. Uongozi wa kiraia na kijeshi unalinda ukuu wa mfumo wa kilimwengu wa kikoloni wa Amerika. Ni wakati sasa wa kukomesha siasa hizi za ubinafsi na mfumo wa kidemokrasia wa kisekula. Umewadia  wakati wa kuweka msingi wa siasa mpya na dola mpya, ambayo inatengeneza maisha yetu kwa mujibu wa Wahyi wa Mwenyezi Mungu (swt). Ni wakati sasa wa kusimamisha Khilafah kwa Njia ya Utume. Katika Khilafah, utiifu na uaminifu kwa Khalifa hutolewa tu ili atawale kwa sheria zilizoteremshwa na Mwenyezi Mungu (swt). Waislamu wote wanamhisabu Khalifa kwa msingi kwamba yeye anaangalia mambo ya watu, kupitia utabikishaji kamili na wa kina wa Uislamu. Idara ya mahakama ya Khilafah hufanya maamuzi kwa misingi ya hukmu za Shariah. Taasisi zote za dola, na watu, hujisalimisha kikamilifu chini ya utukufu wa Shariah. Uamuzi wa Qur'an Tukufu na Sunnah za Mtume ni wa mwisho.

Enyi Waislamu wa Pakistan! Hizb ut Tahrir ndicho chama pekee kinachoweza kukupelekeni kwenye mafikio ya Khilafah. Ndicho chama kinachokuongozeni kwa msingi wa Uislamu pekee. Kamwe hailegezi msimamo fikra na mwelekeo wake, kwa sababu chimbuko la fikra yake ni Uislamu, ilhali njia yake imeegemezwa kwenye nususi za Shariah. Msimamo wake wenye maadili katika miongo kadhaa ya mapambano ni kielelezo cha anga yake safi ya ndani, iliyotakaswa na Iman. Uongozi wake wa kiulimwengu una uwezo kamili wa kushughulikia mambo yenu, kwa kuzingatia maamrisho ya Kiislamu, ambayo Hizb imeeleza kwa kina katika machapisho yake. Kwa hivyo chukueni jukumu lenu kusimamisha Khilafah, sambamba na Mashababu wa Hizb ut Tahrir. Wekeni nia thabiti kwamba hamtapumzika, mpaka jua la Khilafah liumulike Ummah, kwa mara nyingine tena.

Enyi Waislamu wa Jeshi la Pakistan! Demokrasia nchini Pakistan inakusageni katikati ya makundi mawili. Kwa upande mmoja, kuna uongozi wa kijeshi ambao unatumia mamlaka yenu dhidi ya watu wenu. Kwa upande mwingine, kuna wadai wa uongo wa ukuu wa kiraia, ambao wanakulengeni kwa ajili ya mamlaka. Ni Demokrasia hiyo hiyo iliyowakutanisha Waislamu kwa Waislamu katika vita vya Marekani dhidi ya "ugaidi," kwa miongo miwili. Malizeni upotevu wa damu na jasho lenu kwa viongozi wenye ubinafsi. Je, hamtaki kwamba damu na jasho lenu litumike kwa ajili ya utukufu wa Dini ya Mwenyezi Mungu (swt)? Komesheni uhamasishaji dhidi ya watu wenu mwenyewe. Je, hamtamani kuhamasishwa, kunyanyua takbira, kuikomboa Kashmir na Al-Masjid Al-Aqsa?! Je, ukuu wa kijeshi unawezaje kuwa ndio chanzo cha heshima kwenu, wakati unaunga mkono amri ya Magharibi inayopigana vita na Dini yetu? Heshima iko tu katika kumtii Mwenyezi Mungu (swt). Jitokezeni na muupe Nusrah uongozi wa Hizb ut Tahrir kwa ajili ya kusimamisha Khilafah kwa Njia ya Utume. Hakika ni Khilafah Rashida ndiyo itakayozifariji nyoyo za waumini. Ni Khilafah Rashida ndiyo itakayoziunganisha nyoyo zilizogawanyika kupitia nuru ya Uislamu, kama vile Uislamu ulivyoziunganisha nyoyo za makabila na makundi ya al-Madinah al-Munawwarah.

[وَاعْتَصِمُواْ بِحَبْلِ اللّهِ جَمِيعًا وَلاَ تَفَرَّقُواْ وَاذْكُرُواْ نِعْمَةَ اللّهِ عَلَيْكُمْ إِذْ كُنتُمْ أَعْدَاء فَأَلَّفَ بَيْنَ قُلُوبِكُمْ فَأَصْبَحْتُم بِنِعْمَتِهِ إِخْوَانًا وَكُنتُمْ عَلَىَ شَفَا حُفْرَةٍ مِّنَ النَّارِ فَأَنقَذَكُم مِّنْهَا كَذَلِكَ يُبَيِّنُ اللّهُ لَكُمْ آيَاتِهِ لَعَلَّكُمْ تَهْتَدُونَ]

Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye akakuokoeni nalo. Namna hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni Ishara zake ili mpate kuongoka.” [Surah Aali Imran 3:103]

H. 29 Shawwal 1444
M. : Ijumaa, 19 Mei 2023

Hizb-ut-Tahrir
Wilayah Pakistan

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu