Ijumaa, 10 Shawwal 1445 | 2024/04/19
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Tuzo ya Nobel ya Profesa Gurnah isukume Tanzania kujali Wananchi wake

Habari:

Siku ya alkhamis 07/10/2021 Profesa mstaafu wa lugha ya Kiingereza na fasihi baada ya ukoloni na mwandishi wa riwaya Abdulrazak Gurnah alishinda tuzo ya Nobel katika fasihi yenye thamani ya medali ya dhahabu na pesa milioni 10 krona za Uswidi (dolari milioni 1.14) baada ya kutambuliwa mchango wake katika fasihi kutokana na kazi zake za uandishi kuhusu “maisha ya baada ya ukoloni na kiwewe cha uzoefu wa ukimbizi”

Maoni:

Profesa Gurnah(73) anayeishi Uingereza, alizaliwa Zanzibar mwaka 1948 na aliwasili Uingereza mwaka 1968 kama mkimbizi baada ya kukimbia mauaji ya Waislamu nchini Zanzibar hususan Waislamu waliokuwa na asili ya Asia na Arabuni yaliyotokea mwaka 1964 na baada ya hapo. Ametunga riwaya 10 pia ni Mwafrika wa 7 kushinda tuzo hiyo ya Nobel katika fasihi.

Machafuko na vurugu za Zanzibar za mwaka 1964 zilipelekea mauaji ya maelfu, jamii kupotezwa na mamia kufungwa yakihusishwa na yaliyoitwa “mapinduzi ya Zanzibar na athari zake. Watu wengi walikuwa wahanga miongoni mwao ni Profesa Gurnah ambaye hakuwa na jinsi isipokuwa kukimbilia Uingereza miaka ya mwisho ya 1960 akitoroka utawala wa ukandamizaji uliotesa jamii ya Waislamu wenye asili ya Arabuni ambayo (Gurnah) alikuwa anatokea” (The Washington Post 07/10/ 2021)

Profesa Gurnah kutoroka nchi yake aliyozaliwa na kukimbilia Uingereza akikimbia mateso inaonesha wazi jinsi ambavyo serikali zenye uhuru wa bendera za Afrika zilivyo za katili, kidikteta na kibaguzi kwa watu wake wasio na hatia.

Kwa bahati mbaya sana watu ambao wanaitwa wapigania uhuru wa Afrika walikuwa kiuhalisia vibaraka wa Wakoloni Wamagharibi, badala ya kuunganisha watu pamoja baada ya uhuru wao walifanya mauaji yasiyosemekana, mauaji ya halaiki na kuchinja watu wao wenyewe kwa chuki za kibaguzi, malengo yao ya kisiasa na kuwaridhisha mabwana zao Wakoloni Wamagharibi.

Inakadiriwa katika mauaji ya Zanzibar ya mwaka 1964 idadi ya vifo ilifikia takriban watu 20,000 wasio na hatia wengi wao wakiwa ni Waislamu wenye asili ya Asia na Arabuni. Kufuatia mauaji ya kibaguzi, mateso, ubakaji, na kuporwa mali zao, maelfu walijitoa muhanga na kukimbia nchi, walionusurika waliwekwa katika makambi na baadaye kulazimishwa kufukuzwa nchini. (The 1964 Zanzibar Genocide: The Politics of Denial, 2015)

Tabia hii mbaya na chafu ya kuua watu wasio na hatia kwa ajili ya madaraka katika miaka ya 1960 kwa kiasi kikubwa ilihamasishwa na Uingereza. Hata hivyo hali hii bado inaendelea kufanyika mpaka leo hii.

Kwa mfano, katika miaka ya 2000, polisi wanatuhumiwa kuua waandamanaji 35 na kujeruhi 600 Zanzibar kufuatia maandamano baada ya uchaguzi. Askari na mgambo wa chama tawala CCM walitembea nyumba hadi nyumba wakiwasaka na kuwakamata watu waliowahisi ni wafuasi wa upinzani na kusababisha takriban watu 2000 kukimbilia nchini Kenya. (The Political Crisis in Zanzibar, 2016)

Mwaka 2012 wanachama na viongozi wa taasisi ya Uamsho walikamatwa na kisha kusafirishwa mpaka Tanzania bara kisha wakafunguliwa mashtaka ya uongo ya kubambikiziwa ya ugaidi. Baada ya miaka zaidi ya 7 ya kuwawekwa kizuizini na mateso wakaachiwa mwaka 2021 baada ya serikali kushindwa kwa zaidi ya miaka 7 ya upelelezi wao kuleta ushahidi dhidi yao. Hii ni zaidi ya aibu!

Ukandamizaji wa watu wasio na hatia hususan Waislamu haukuishia Zanzibar pekee bali ulivuka mipaka na kuingia Tanzania bara ambapo mamia kama si maelfu ya Waislamu wengi wao wakiwa hawana hatia wamewekwa vizuizini kwa madai ya uongo ya kubambikiziwa ya ugaidi na kuhatarisha usalama wa nchi kutokana tu na chuki za kidini, kuwaridhisha Wakoloni Wamagharibi na kupata hongo kutoka kwa Wakoloni kwa jina la fedha za kupambana na ugaidi.

Suala hili limewaathiri wengi katika Waislamu; masheikh, maustadh, wanaharakati na Waislamu wa kawaida ambao wamewekwa vizuizini kwa miaka mingi  kwa kisingizio cha “upelelezi haujakamilika”. Kwa mfano mwaka 2017 wanachama watatu wa Hizb ut Tahrir Tanzania; Ustadh Ramadhan Moshi Kakoso, pamoja na Omar Salum Bumbo na Waziri Suleiman Mkaliaganda walitekwa wakawekwa kizuizini kisha wakabambikiwa kesi ya ugaidi na kuna Waislamu wengine wengi katika mikoa mbalimbali nchini kama vile Tanga, Mwanza, Arusha, Lindi, Pwani, nk wote hawa wamewekwa vizuizini kwa miaka mingi bila ya uthibitisho wa madai dhidi yao.

Ni muda muwafaka kwa Tanzania, pande zote mbili za muungano yaani Zanzibar na Tanganyika kujifunza kutokana na kadhia hii kuwa badala ya kushangilia na kujisifu kwa ushindi wa Profesa Gurnah, mara moja waache kukandamiza na kutesa watu wao wasio na hatia hususan Waislamu.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu