Jumanne, 09 Ramadan 1445 | 2024/03/19
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC): Chombo Mikononi mwa Marekani

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) iliyo jijini The Hague/ Uholanzi imetoa agizo la kukamatwa kwa Rais wa Urusi Vladimir Putin.

Maoni:

Wiki hii, ni mwaka wa 20 baada ya uvamizi wa kikatili wa Iraq ulioongozwa na Marekani na Uingereza. Vita hivyo, vilivyosababisha vifo vya mamia kwa maelfu ya raia, vilitokana na udanganyifu na uongo mtupu kwamba Iraq chini ya Saddam Hussein ilikuwa na silaha za maangamizi makubwa (WMD). Matokeo yake: iliwaacha wengi wamekufa, nchi isiyo na utulivu, eneo ambalo lingali na machafuko na kusema "pole" ya rahisi ya wahalifu wa vita hivyo.

Leo Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) huko The Hague/ Uholanzi, ambayo Marekani ilicheza dori kubwa katika kuasisiwa kwake, imetoa agizo la kukamatwa kwa Rais wa Urusi Vladimir Putin kwa vita vyake nchini Ukraine. Rais wa Marekani Biden alisema kuwa rais huyo wa Urusi "amefanya uhalifu wa wazi wa kivita" na kusema kwamba kibali cha kukamatwa kutoka kwa ICC 'ni cha haki.'

Hata hivyo, Marekani haiitambui mahakama hiyo ambayo imeunda. Iliianzisha mahakama hiyo na baadaye kujiondoa kutoka kwayo na hata kufanya kazi kwa uchangamfu kuhujumu mamlaka yake. Wakati Marekani imeunga mkono kufunguliwa mashtaka kwa wahalifu wa kivita kutoka nchi nyengine, imekataa kuwaweka wanajeshi wake na maafisa wake chini ya mamlaka ya ICC. Pia, haitambui mamlaka ya ICC kuchunguza au kuwashtaki raia wa Marekani kwa uhalifu uliofanywa nje ya Marekani. Aidha, Marekani inaingilia kazi ya ICC. Kwa mfano, Marekani imetishia kuchukua hatua dhidi ya maafisa wa ICC na imelazimisha vikwazo kwa watu wanaohusishwa na mahakama hiyo.

Hali hiyo hiyo inatekelezeka kwa nchi za Magharibi ambazo tofauti na Marekani ziliidhinisha Mkataba wa Roma na kuitambua ICC, kama Uingereza. Kwa hivyo, kinadharia, Uingereza inalazimika kushirikiana na ICC na kutii maamuzi na hukumu za mahakama hiyo. Hata hivyo, Uingereza pia imeelezea wasiwasi wake kuhusu mamlaka ya ICC na imechukua hatua kulinda maslahi yake ya kijeshi na kisiasa, hasa kuhusiana na uwezekano wa uchunguzi wa ICC na kufunguliwa mashtaka kwa raia wa Uingereza. Kwa hivyo, ikitafsiriwa kwa ukweli halisi: hapakuwa na agizo la kukamatwa lililotolewa na ICC dhidi ya Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza Tony Blair au kwa maafisa wengine wa Uingereza kwa uhalifu wao wa kivita walioutendwa nchini Iraq. Mnamo 2016, Uchunguzi wa Chilcot, uchunguzi wa serikali ya Uingereza juu ya dori ya Uingereza katika Vita vya Iraq, ulihitimisha kwamba Blair alizidisha kesi ya vita na kwamba ushiriki wa Uingereza uliegemezwa juu ya msingi wa ujasusi mbovu na mipango isiyotoshelevu. Lakini ripoti hiyo ya Chilcot haikutoa matokeo yoyote ya kisheria au mapendekezo ya kufunguliwa mashtaka na hadi leo, hakujakuwa na mashtaka ya jinai au uchunguzi wa ICC dhidi ya Blair dhidi ya uhalifu wa kivita nchini Iraq.

Marekani na nchi nyingine za Magharibi zinatekeleza kibaguzi "sheria ya kimataifa" ambazo wao wenyewe ndio walioziunda. Wanaipinda kwa urahisi, kuipuuza, au kuitumia kutumikia maslahi yao wenyewe, na haswa inapokuja kwa maslahi ya Marekani. Wanayatiisha mataifa mengine kuzifuata ilhali sheria hizi hazina athari yoyote kwao: wengine wanawajibika kwa matendo yao, lakini hawawajibishwi. Hili linaifanya ICC na ile inayoitwa sheria ya kimataifa na kanuni za Mkataba wa Umoja wa Mataifa na kadhalika, kuwa chombo mikononi mwa madhalimu wa leo.

Kwa wakati huu, wahalifu hawa wanaweza kukwepa na uhalifu wao wa kivita, mauaji ya halaiki na uhalifu dhidi ya binadamu. Amesema Mwenyezi Mungu (swt):

[وَلاَ تَحْسَبَنَّ اللّهَ غَافِلاً عَمَّا يَعْمَلُ الظَّالِمُونَ إِنَّمَا يُؤَخِّرُهُمْ لِيَوْمٍ تَشْخَصُ فِيهِ الأَبْصَارُ]

“Wala usidhani Mwenyezi Mungu ameghafilika na wanayo yafanya madhaalimu. Hakika Yeye anawaakhirisha tu mpaka siku yatapo kodoka macho yao.” [Ibrahim: 42]. Lakini si muda mrefu, utawala ujao wa Khilafah Rashida kwa njia ya Utume utaleta nuru na uadilifu kwa ulimwengu baada ya ulimwengu kutumbukia kwenye giza na dhulma, na utawahesabu wahalifu na madhalimu wa kisasa kwa dhulma, ukandamizaji na umwagaji damu wao.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Okay Pala
Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari wa Hizb ut Tahrir Uholanzi

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu