Jumamosi, 11 Shawwal 1445 | 2024/04/20
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Jibu la Swali

Ukweli wa Mvutano kati ya Uturuki na Ugiriki, Hasa Mzozo juu ya Visiwa vya Bahari ya Aegean.

(Imetafsiriwa)

Swali:

Katika taarifa ya mwisho iliyotolewa na Umoja wa Ulaya katika mkutano wake wa kilele jijini Brussels tarehe 23-24/6/2022, chini ya jina la "Mediterrania ya Mashiriki" kuhusiana na uhusiano wa Uturuki na Ugiriki, hasa mzozo wa visiwa vya Bahari ya Aegean: ["Umoja wa Ulaya inaelezea wasiwasi mkubwa juu ya kauli na hatua za Uturuki hivi karibuni, Uturuki inapaswa kuonyesha heshima kwa mamlaka na uadilifu wa eneo la nchi zote wanachama wa EU..." (VOA 24/6/2022)]. Kwa upande mwingine, Uturuki ilisema katika taarifa iliyochapishwa na Wizara yake ya Mambo ya Nje, "Kufikia msimamo ambao ni wa upendeleo, usio na maono na tofauti na ukweli kuhusu nchi yetu katika maamuzi yaliyopitishwa wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali za Muungano wa Ulaya, inasikitisha, na haikubaliki kwa Umoja wa Ulaya kujaribu kuhalalisha mapendekezo yenye msimamo mkali ambayo yanakiuka sheria za kimataifa kuhusu Mediterania ya Mashariki na Bahari ya Aegean..." (Anatolia 24/6/2022)]. Je, hii ina maana kwamba mvutano umerejea kwenye uhusiano kati ya Uturuki na Ugiriki tena? Je, hii inaweza kusababisha vita kati yao ingawa wote wako katika NATO? Pia, Marekani ina msimamo gani inapoongoza muungano huu? Je, inaweza kuondoa mvutano huu na kutuliza mambo, au mvutano huu utaendelea kuongezeka?

Jibu:

Ili kufanya jibu kuwa wazi, hebu tupitie mambo yafuatayo:

1- Kuna takriban visiwa 1,800 vidogo na vikubwa na miundo ya miamba katika Bahari ya Aegean, karibu 100 ambayo inakaliwa na visiwa 24 tu vyenye eneo la zaidi ya 100 km2. Visiwa hivi vilianza kuwa chini ya himaya ya Uislamu na mamlaka ya Waislamu pamoja na nchi za Ugiriki tangu Muhammad Al-Fatih, Mwenyezi Mungu amrehemu, alipoanza ushindi humo kuanzia mwaka 1456 M baada ya ushindi mkubwa wa Istanbul mji mkuu wa mashariki wa Warumi mnamo 1453 M. Lakini wakati udhaifu ulipoanza kuonekana kwenye Dola ya Kiuthmani kama Dola ya Kiislamu, nchi za Kikafiri zilichukua fursa ya hali hiyo na kuanza kula njama dhidi ya Dola ya Kiislamu, na kuwachochea Wagiriki kuasi dhidi yake.

Badala yake, Uingereza, Ufaransa na Urusi ziliingilia moja kwa moja vita vya majini dhidi yake ili kuitenganisha Ugiriki kutoka kwayo hadi hili lilipotukia mwaka 1830 M. Lakini mamlaka juu ya vingi ya visiwa hivyo ilibakia kwa Dola la Kiuthmani, hadi Italia ilipoteka Visiwa vya Dodecanese mwaka wa 1912 M wakati wa vita vya Libya, ambavyo vinaitwa Visiwa 12, ambavyo hapo awali vilikuwa visiwa 14, pamoja na visiwa kumi vidogo na vilima vya mawe.

Visiwa hivi vilipata umuhimu kwa sababu viko karibu na mipaka ya Uturuki baada ya kugawanywa kwa Mkataba wa Lausanne. Baadhi viko umbali wa kilomita 3 hivi kutoka kwenye mipaka ya Uturuki, ilhali viko takriban kilomita 500 kutoka pwani ya karibu ya Ugiriki. Visiwa hivi vilipewa Italia katika Mkataba wa Lausanne, ambao ulitiwa saini na serikali ya Ankara iliyoongozwa na Mustafa Kemal kupitia mjumbe wake Ismet Inonu, ambapo waliachia maeneo makubwa ya Dola ya Kiuthmani na kuridhika na ile inayoitwa Uturuki ya sasa, iliyowekwa na washirika wakiongozwa na Uingereza. Italia ilishinda utambuzi wa Uingereza wa haki yake ya visiwa hivyo kwa kurudi kuingia Vita vya Kwanza vya Dunia kwa upande wake dhidi ya Ujerumani na Dola ya Kiuthmani. Mnamo 1947, makubaliano ya amani yalitiwa saini jijini Paris kati ya Dola za Washirika na Italia, baada ya kushindwa katika Vita vya pili vya Dunia. Makubaliano hayo yalibainisha kuwa Italia itakabidhi Visiwa vya Dodecanese, Visiwa 12, kwa Ugiriki, kwa sharti kwamba vitaondolewa kijeshi. Uturuki inadai mazungumzo ili kujua hatima ya visiwa vingi vinavyozozaniwa, na visiwa vidogo ambavyo havihusiani na nchi yoyote chini ya makubaliano ya hapo awali, wakati Ugiriki inadai haki yake kwa visiwa vyote vya Bahari ya Aegean, isipokuwa kwa visiwa vingine vilivyorejeshwa kwa Uturuki chini ya Mkataba wa Lausanne pekee.

Ugiriki inaomba kuongeza maji ya eneo lake kutoka maili 6 hadi maili 12. Uturuki bado iko chini ya na kuidhinisha Mkataba wa Paris, ingawa haikuwa sehemu yake na haikutia saini! Waziri wake wa Mambo ya Nje Cavusoglu alisema katika mahojiano na Gazeti la Al-Hurriyat mnamo tarehe 26/5/2022, "Ugiriki lazima ifuate mkataba wa amani uliohitimishwa mwaka 1947, ambao unaruhusu kikosi kidogo tu cha kijeshi cha wanajeshi wa Ugiriki kuwepo kwenye Visiwa vya Dodecanese. " "Waziri alionya kwamba hali itaongezeka ikiwa Ugiriki haitatii masharti ya mkataba wa amani." Mwelekeo mwingine wa mgogoro unahusiana na haki zinazotokana na mamlaka hiyo, ambayo inawakilishwa katika nyanja za ushawishi wa baharini na maeneo ya kiuchumi, na haki ya kuchunguza rasilimali za nishati kama vile mafuta na gesi karibu na visiwa hivi. Kwa hili liliongezwa suala la kuanzisha misingi ya Marekani juu yao, pamoja na matarajio ya Ulaya na hasa Ufaransa katika eneo hili.

2- Ufaransa ilijiunga na kuonyesha wazi uungaji mkono wake kwa Ugiriki dhidi ya Uturuki. Ilitangaza kuunga mkono Ugiriki dhidi ya Uturuki katika majira ya joto ya 2020, na kutuma ndege za Rafale na manuari kukabiliana na kuenea kwa meli za kijeshi na kazi ya uchunguzi wa Kituruki mashariki mwa Mediterania. Ilitia saini na Ugiriki makubaliano ya ushirikiano wa pande zote mnamo Septemba 2021, ambayo yaliweka "msaada wa pande zote kwa njia zote zinazofaa ikiwa nchi hizo mbili zitagundua kwa pamoja kuwa shambulizi la silaha linafanyika dhidi ya eneo la mmoja wao." Ufaransa iliimarisha makubaliano hayo na kutia saini makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi wa pamoja kati ya nchi hizo mbili mnamo Januari 2022, ikisisitiza kwamba "ushirikiano wa kimkakati unaunganisha nchi hizo mbili katika kiwango cha kijeshi," kulingana na taarifa ya Mkuu wa majeshi ya Ufaransa. Makubaliano haya pia yanaruhusu "kuimarisha na kupanga mahusiano ya ulinzi na kijeshi kwa muda mrefu, na mfano wa ushirikiano wa kijeshi kati ya Ufaransa na Ugiriki katika ngazi za kimkakati na uendeshaji. Na kwamba ushirikiano wa kijeshi kati ya nchi mbili hizi utapanuliwa." ( France Press 22/1/2022) Siku mbili kabla ya kusainiwa kwa mkataba huu, Ugiriki ilitangaza kupokea wapiganaji 6 wa Rafale kutoka Ufaransa kati ya ndege 18 za kivita za Rafale ambazo Ugiriki ilitangaza kuzinunua kutoka Ufaransa mwaka jana. Mbali na frigate 3, yenye thamani ya euro bilioni 5.5, wataalam walinukuliwa na AFP wakisema, "Mkataba huu wa ulinzi haujawahi kutokea na sio wa kawaida, kwa sababu unaunganisha nchi mbili wanachama wa NATO na unalenga Uturuki, mwanachama mwingine wa muungano." Ufaransa ilishawishi Umoja wa Ulaya na msimamo huu na msimamo wake ulipendelea Ugiriki dhidi ya Uturuki.

3- Amerika haikukaa kimya juu ya hatua hii ya Ufaransa, kwa hivyo ilihamia kubatilisha athari yake na kuelekeza pigo la kwanza kwa Ugiriki. Cyprus, Ugiriki na umbile la Kiyahudi zilitangaza mnamo tarehe 20/12/2018 nia yao ya kuanzisha mradi wa bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka mashariki mwa Mediterania hadi Ulaya bila Uturuki na sehemu ya kaskazini ya Uturuki ya Cyprus kuwa na mchango katika hilo. Bomba hili lilitakiwa kupata takriban mita za ujazo bilioni 10 za gesi asilia hadi Ulaya. Lakini Amerika ilitangaza mwisho wa msaada wake kwa mradi huo. Iliarifu umbile la Kiyahudi na Ugiriki mnamo 10/1/2022 kwamba "haitaunga mkono mradi huo kisiasa na kifedha." Huu ulionekana kuwa "ushindi kwa Uturuki, ambayo ulitengwa na mradi huo" (Al-Sharq Al-Awsat 10/1/2022), na Jarida la Kijeshi la Ugiriki lilionyesha katika ripoti iliyochapishwa mnamo 10/1/2022 na akisema:

(“Mradi wa Athens wa kuongeza ushawishi wa kisiasa wa kijiografia ili kuwa kitovu cha nishati na muungano wa kihistoria na 'Israel' ambao ulisababisha kutengwa kwa Uturuki na kufikiwa kwa malengo mengine kuporomoka kabisa... Hali hiyo hiyo inatumika kwa Sheria ya Manyatis, ambayo inafafanua mipaka ya nje ya rafu ya bara la Ugiriki. Malengo yote mawili yaliporomoka, na Uturuki ikavunja Sheria ya Manyatis, ambayo inaiita ‘Blue Home’, na imeimarisha ukuu wake juu ya nafasi za Ugiriki kwa makubaliano ya Uturuki na Libya, na sasa msimamo wa Washington imekuja kuipa fursa hiyo.” Ilisema, "Waziri Mkuu wa Ugiriki Mitsotakis hataki kufanya mazungumzo na Uturuki... vile vile hakufanya mazungumzo na Amerika..." Iliongeza kuwa "Marekani ilifanya kazi kupitia Ujerumani ili kuzuia kuwekewa vikwazo Uturuki kutokana na mzozo wa uchimbaji visima katika eneo la mashariki mwa Mediterania mwaka jana.” Tukiangalia kwa makini suala hilo, tunaona kwamba Marekani ilitaka kuelekeza pigo kwa Ugiriki kwa ushirikiano wake na Ufaransa na kubatilisha athari za hatua ya Ufaransa katika eneo hilo, na Amerika ilitaka kuunganisha mradi huo na Uturuki, mshirika wake wa karibu, ambayo inazunguka katika mzunguko wake ili kukabiliana na Ufaransa.

4- Ugiriki ilitambua kuwa 'iliikasirisha' Marekani kwa makubaliano yake na Ufaransa na maelewano yake nayo, na ili kurekebisha suala hili, ilikubali kutia saini makubaliano na Amerika kwamba Bunge la Ugiriki lilikuwa limeakhirisha saini yake kutoka 14/10/2021 hadi 13/5/2022, ilipotiwa saini. Wakati wa kura hiyo, Waziri Mkuu wa Ugiriki Mitsotakis alitetea makubaliano hayo, na kusema: “Makubaliano ya ushirikiano wa kiulinzi na Marekani yanahudumia maslahi ya kitaifa ya nchi. Ni kura ya imani kwa Ugiriki, na ni muhimu kwa sababu kwanza: inajumuisha ahadi ya wazi kwamba uwepo wa Marekani nchini Ugiriki utafanywa upya kila baada ya miaka 5 (badala ya mwaka mmoja kama hapo awali), kila upande una haki ya kusitisha ukiona ni lazima.

Pili: Ushirikiano huu baina ya nchi mbili hizi na Marekani ni muhimu kwa sababu unapanuka sio tu kwa wakati ufaao bali pia mahali pake. Katika Kituo cha Nevi cha Souda (huko Krete), miundombinu yote inafanywa kuwa ya kisasa na dori jumla ya kambi inaimarishwa. Souda ndio bandari pekee ambayo meli inayobeba ndege za Marekani inaweza kutia nanga mashariki mwa Mediterania, pamoja na masafa ya kurusha risasi huko Litochoro na kambi mbili za kijeshi huko Volos na Alexandroupolis. Tatu, makubaliano hayo mapya ni muhimu kwa sababu yanaonyesha wazi nia ya pamoja ya kulinda mamlaka na uadilifu wa eneo kutokana na tishio lolote, hata shambulizi la silaha." (Siku ya Saba kupitia mashirika ya habari 5/13/2022).

Kwa hivyo, Amerika iliitiisha Ugiriki kwa matakwa yake, ikaimarisha ushawishi wake ndani yake, na ikalemaza ushirikiano wake na Ufaransa!

5- Baadaye, kauli za Ugiriki zilitulia, na Waziri Mkuu wa Ugiriki alisema ["Ni muhimu kuweka njia za mawasiliano na Uturuki wazi, licha ya kauli za kuudhi zilizosababisha kuongezeka kwa mvutano kati ya majirani hao wawili." (The New Gulf 17/6/2022)]. Lakini hali hii imeuweka Muungano wa Ulaya matatani! Kwa hivyo, ili kuokoa uso, iliridhika na tamko la jumla la upole kuelekea Uturuki huku ikionyesha uungaji mkono kwa Ugiriki kama mwanachama wa Muungano: (Taarifa ya mwisho iliyotolewa katika mkutano wake wa kilele jijini Brussels mnamo 23 na 24/6/2022 chini ya kichwa. "Mediterania ya Mashariki" ilisema: Umoja wa Ulaya ulionyesha wasiwasi wake mkubwa juu ya kauli na hatua za hivi karibuni za Uturuki, Uturuki inapaswa kuonyesha heshima kwa ubwana na hadhi ya kieneo kwa nchi zote wanachama wa EU.)

Baadaye, Waziri Mkuu wa Ugiriki alisema: "Tunasimama kikamilifu nyuma ya kile kilichosemwa katika taarifa ya mwisho ya Muungano wa Ulaya, ambayo iliifanya Uturuki iwajibike kuhusu ubwana na heshima ya kieneo ya wanachama wa Muungano wa Ulaya na kutaka kupunguza mvutano kwa mujibu wa sheria za kimataifa. Natumai kwamba wakati huu Uturuki itatii wito huu... kwa sababu hiyo ndiyo njia pekee ya kupunguza kabisa mvutano ambao umeongezeka na jirani yetu katika kipindi cha miezi miwili iliyopita katika eneo la mashariki mwa Mediterania” (Voice of Amerika 24/6/2022).

6- Kwa hivyo, Amerika iliweza kupunguza mvutano kati ya Uturuki na Ugiriki, wakati Uturuki inazunguka katika duara lake, na Ugiriki imeshikiliwa na makubaliano ya ulinzi na Amerika, na ushawishi wa Muungano wa Ulaya, haswa Ufaransa, kwa Ugiriki umepungua, na hivyo haiwezekani kwamba mgogoro wa kisiwa katika Bahari ya Aegean, ikiwemo visiwa vya Dodecanese, utakuwa na ufumbuzi wowote kwa muda mrefu. Itabaki kama ilivyo kwa miaka kadhaa. Kwa hakika, utawala wa Uturuki umetambua kwa uwazi kupeanwa kwa Visiwa 12 kwa Ugiriki katika Mkataba wa Paris wa 1947. Utawala huu hauna mpango wa kuvirudisha, pamoja na visiwa vyengine ambavyo umiliki wa Ugiriki haukuamuliwa rasmi katika makubaliano. Utawala wa kisekula wa Uturuki hautarajiwi kuchukua hatua kali kuvirejesha visiwa hivi katika Bahari ya Aegean, ambayo inadhibitiwa na Ugiriki. Erdogan hafanyi chochote isipokuwa vita vya maneno, na kisha kurudi nyuma, kama ilivyotokea mnamo 2020, wakati alipoondoa meli za kuchimba visima mashariki mwa Mediterania, na pazia ikashuka juu ya suala hilo. Kwa hivyo, haitarajiwi kwamba kutakuwa na vita kati ya Uturuki na Ugiriki, ili kurejesha visiwa hivi, kwani minyororo ya suala hilo iko mikononi mwa Amerika, na Uturuki inazunguka ndani ya duara lake, na Ugiriki baada ya makubaliano hayo, imeona ushawishi wa Amerika ukiongezeka ndani yake.

7- Hatimaye, visiwa vya Bahari ya Aegean, na hata Ugiriki, vilikuwa ndani ya Dola ya Kiislamu (Uthmani). Baada ya kutekwa kwa Konstantinopoli mnamo 1435 M, kufikia Hadith ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw):

«لَتُفْتَحَنَّ الْقُسْطَنْطِينِيَّةُ فَلَنِعْمَ الْأَمِيرُ أَمِيرُهَا وَلَنِعْمَ الْجَيْشُ ذَلِكَ الْجَيْشُ»

“Itafunguliwa Konstantinopli na Amiri wake ndiye amiri bora na jeshi lake ndilo jeshi bora.” [Imetolewa na Ahmad katika Musnad yake].

Baada ya miaka mitatu, yaani, mwaka 1456 M, ushindi ulielekea Ugiriki na kuelekea visiwa hivyo, ambapo mwito wa swala (Allahu Akbar Allahu Akbar) ulipazwa. Itarejea, Mwenyezi Mungu akipenda, siku ambayo Waumini watafurahia ushindi wa Mwenyezi Mungu, Khalifa atakapowaongoza Waumini, atawatawala kwa yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, na atawaongoza katika Jihad katika njia ya Mwenyezi Mungu (swt). Na atarejesha makaazi ya Uislamu, asili na matawi yake. Khalifa ni ngao ya Ummah na kinga dhidi ya maadui zake, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema:

«إِنَّمَا الْإِمَامُ جُنَّةٌ يُقَاتَلُ مِنْ وَرَائِهِ وَيُتَقَى بِهِ»

“Hakika Imam ni ngao watu hupigana nyuma yake na hujihami kwake.” [Muslim].

5 Dhul Hijjah 1443 H

4/7/2022 M     

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu