Alhamisi, 18 Ramadan 1445 | 2024/03/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vipi Khilafah Itakavyo Unda Nidhamu ya Elimu ya Daraja ya Juu Kabisa

Allah (swt) asema,

(الَر كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ لِتُخْرِجَ النَّاسَ مِنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ بِإِذْنِ رَبِّهِمْ إِلَى صِرَاطِ الْعَزِيزِ الْحَمِيدِ)

“Alif Lam Ra. (A. L. R) Hichi ni Kitabu tulicho kiteremsha kwako ili uwatowe watu kwenye giza uwapeleke kwenye muwangaza, kwa idhini ya Mola wao Mlezi, uwafikishe kwenye Njia ya Mwenye nguvu, Msifiwa.” [Ibrahim: 1]

• Ili kuunda Nidhamu ya Elimu ya Daraja ya Juu Kabisa ya aina hiyo yahitaji nidhamu ya kisiasa ya daraja ya juu kabisa – nidhamu inayo kumbatia ruwaza ya kisiasa ya kipekee, ya hali juu na huru kwa dola yake na kwa ulimwengu, iliyo jengwa kwa msingi wa ayah hiyo ya juu – kuwatoa watu kutoka katika giza la ujinga wa ukafiri na kuwapelekea katika nuru ya Uislamu na uadilifu na mafanikio unayoleta kwa wanadamu katika kila nyanja ya maisha – kiroho, kiakili, kiakhlaqi, kisiasa, kiuchumi, na katika sayansi na teknolojia.

Nidhamu hii ya kisiasa ya daraja ya juu kabisa ni Khilafah kwa njia ya Utume inayo tabikisha imani, sheria na nidhamu za Kiislamu kwa ukamilifu juu ya dola, na ambayo kwa karne kadhaa iliongoza dunia katika mafanikio ya taasisi zake za kielimu na ubunifu na uvumbuzi wake wa kipekee, pamoja na mchango wake mkubwa kwa maendeleo ya binadamu.

• Khilafah itaasisi nidhamu ya elimu ya daraja ya juu kabisa iso na kifani itakayo kuza kizazi cha vijana na kuunda Ummah na dola zinazojifunga na sifa za kuwaongoza wanadamu kutoka katika giza kwenda katika nuru kama inavyo amrishwa na Mwenyezi Mungu (swt). Haitakubali kubaki nyuma ya mataifa mengine katika mafanikio ya kimasomo wala kukubali daraja yoyote ya pili ya nidhamu ya elimu inayofadhiliwa na makombo kutoka kwa dola.  

• Khilafah inawajibishwa na Mwenyezi Mungu (swt) kuwa na ruwaza huru ya kisiasa kindani na kimataifa iliyo jengwa kwa msingi safi juu ya Uislamu; na hivyo pia kuwa huru katika uundaji wa mtaala wake wa elimu, pamoja na utoaji huduma zake za umma na miundo msingi, na ushibishaji mahitaji ya dola na watu wake. Hivyo basi haitakubali kutegemea biladi yoyote ya kigeni katika kuimarisha sekta zake za uchumi, ukulima, viwanda, matibabu, elimu, jeshi, sayansi na teknolojia au sehemu nyengine yoyote ya dola ambayo huianika wazi kwa utumiwaji vibaya na serikali za kikoloni. 

• Khilafah itaasisi ndoa imara kati ya elimu na utekelezaji wa kadhia na maslahi nyeti ya dola na raia wake, ikihakikisha kujitegemea na kujitosheleza – hivyo kuondoa utengano uliopo sasa kati ya nidhamu za elimu katika biladi zetu na mahitaji ya kiviwanda, kiukulima, kiufundi na mahitaji mengineyo ya mujtamaa zetu, inayopelekea kutegemea mataifa mengine. Hili, pamoja na uwekezaji mzito wa Khilafah katika uimarishaji viwanda ili kukidhi mahitaji ya mujtama wake kwa kujitegemea yenyewe na kuifanya dola hiyo kuwa dola kuu duniani, itadhibiti na kutumia ujuzi na akili za kipekee za wahitimu vyuo wa Ummah huu kwa ajili ya maendeleo ya dola hii, ili uwezo wao mwanana usifujwe au kutekwa nyara na serikali za kigeni.  

• Msingi unaofunga vipengee vyote vya nidhamu ya elimu ndani ya Khilafah – kuanzia malengo yake, masomo yanayo fundishwa, maalumati yaliyomo ndani ya mtaala na mafunzo, mpangilio wa shule na kila kitu chengine ni Itikadi ya Kiislamu pekee, kwani Mwenyezi Mungu (swt) asema,

 (وَمَن يَبْتَغِ غَيْرَ الإِسْلاَمِ دِينًا فَلَن يُقْبَلَ مِنْهُ وَهُوَ فِي الآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ)

“Na anayetafuta dini isiyokuwa Uislamu haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa katika wenye kukhasiri.” [Al-e-Imran: 85]

“Ni wajib kuwa Itikadi ya Kiislamu iwe ndio msingi wa mtaala wa elimu. Mtaala na mbinu za ufundishaji zote hutungwa kwa njia isiyo potoka kutoka katika msingi huu.” (Kifungu cha 170, Kielelezo cha Katiba ya Al-Khilafah cha Hizb ut Tahrir)

• Kuna malengo matatu makuu ya Nidhamu ya Elimu ya Khilafah:

(i) Uundaji Shakhsiya ya Kiislamu:

Hili hupatikana kupitia kukuuza Itikadi, fahamu na tabia za Kiislamu ndani ya wanafunzi ili wawe ni Waislamu wanaouchukua Uislamu kuwa ndio msingi wa pekee wa fikra, maamuzi, matamanio na vitendo vyao vyote na kuunda maisha yao yote kwa mujibu wa Dini yao. Lengo hili litasaidiwa na mazingira ya Kiislamu ya Khilafah ambapo vyombo vyake vya habari, misikiti na taasisi zote nyengine hazitapigia debe chochote isipokuwa fahamu safi za Kiislamu. 

(ii) Ufundishaji Ujuzi na Elimu ya Kivitendo kwa Ajili ya Maisha:

Wanafunzi watafundishwa wanachohitaji katika ujuzi na elimu ya kuingiliana na mazingira yao ili kuwatayarisha kuingia katika mzunguko wa maisha ya kivitendo, kama vile hesabu, sayansi jumla na elimu na ujuzi wa kutumia ala na uvumbuzi, kwa mfano vifaa vya umeme na elektroniki, tarakilishi, vifaa vya nyumbani, ala za ukulima na viwanda, na kadhalika. Pia watafunzwa michezo yenye manufaa kama vile kuogelea na ulengaji shabaha, na baada ya kubaleghe watapewa mafunzo ya kijeshi chini ya ishrafu ya jeshi.

(iii) Utayarishaji Wanafunzi Kuingia Vyuo Vikuu:

Wanafunzi watatayarishwa kwa ajili ya kuingia vyuo vikuu kupitia kuwafundisha sayansi msingi zinazo hitajika – iwe za kithaqafa kama Fiqh, Lugha ya Kiarabu, au Tafsiri ya Qur’an, au sayansi za kiutafiti – kama vile hesabu, kemia, bayolojia au fizikia. Lengo ni kuunda shakhsiya, wanazuoni, wanasayansi, na wataalamu wa kipekee katika kila nyanja ya maisha ili kuimakinisha Khilafah kama dola kuu, yenye ushawishi, inayo ongoza duniani. Mbinu za ufundishaji zinazo shajiisha tafakari ya kina zitatumiwa. Sayansi za kiutafiti kwa mfano zitafundishwa kwa njia inayo jenga ujuzi wa kutathmini, na ambapo mada zitatumiwa ili kutatua matatizo halisi ya kimaisha na kufanyiwa utafiti ili kuvua manufaa kutokana nazo ili kutumikia maslahi ya Ummah na kadhia zake nyeti.

Mjumuiko huu jumla wa mtaala wa ufundishaji utaunda mjumuiko jumla wa shakhsiya za Kiislamu zilizo za kipekee katika ufahamu wao wa Dini yao na maumbile ya ulimwengu huu, pamoja na kutayarishwa kwa msingi unao hitajika kuingia katika masomo ya juu.

• Daraja za usomaji shule pia zimeundwa juu ya Itikadi ya Kiislamu kwani zimefungwa kwa msingi wa dalili za Kisheria zinazo husiana na hukmu, majukumu, na adhabu tofauti tofauti za Kiislamu zinazo tekelezwa juu ya mtoto katika umri tofauti tofauti. Kuna daraja 3 za shule – ya kwanza (au daraja ya Msingi) – kuanzia umri wa miaka 6 hadi 10; daraja ya pili (au Shule ya Wastani) kuanzia kukamilisha umri wa miaka 10 hadi 14; na daraja ya tatu (au Shule ya Upili) kuanzia kukamilisha miaka 14 hadi mwisho wa daraja za shule. 

• Hakutakuweko na mchanganyiko baina ya wanaume na wanawake katika taasisi za elimu za dola kama ilivyo fafanuliwa na Uislamu – ima baina ya wanafunzi au walimu.

• Ni jukumu la Kiislamu juu ya Khilafah kutoa ubora wa hali ya juu wa elimu kwa kila mmoja wa raia wake kama haki msingi – bila ya kujali dini, tabaka, jinsia au kiwango chao cha utajiri. Inawajibishwa kuweka shule za kutosha za msingi na upili na kuajiri walimu wa kutosha kwa raia wote wa dola na kuwapa vifaa vyote wanavyo hitaji ili kufikia malengo ya sera ya elimu bila ya malipo.

“Ni jukumu juu ya Dola kumsomesha kila mtu, mwanamume au mwanamke, vile vitu ambavyo ni muhimu katika maisha ya kawaida. Hili lapaswa kuwa wajib na kupeanwa bila ya malipo katika viwango vya elimu ya msingi na upili. Dola inapaswa, kwa kadri ya uwezo wake, kutoa fursa kwa kila mmoja kuendelea na elimu ya juu bila ya malipo.” (Kifungu cha 178, Kielelezo cha Katiba ya Al-Khilafah cha Hizb ut Tahrir)

• Uwekezaji katika elimu utakuwa ndio kipaumbele cha Khilafah. Kama dola inayo tafuta kuongoza dunia na kuwatumikia watu wake na wanadamu wote kwa jumla kwa ikhlasi, haitakubali nidhamu yoyote ya elimu ya daraja ya pili kutokana na ukosefu wa ufadhili. Bali, itatafuta kuunda wingi wa walimu na wahadhiri walio funzwa vyema na wenye kulipwa vizuri, pamoja na shule, vyuo, vyuo vikuu, vituo vya utafiti, maktaba, maabara na nyengine zaidi za kisasa, zenye vifaa vya kutosha, kwa kutumia mali ya Hazina yake Kuu (Bait ul-Mal), ambayo mali zake inshaAllah zitakuwa nyingi mno kutokana na umbile sahihi la nidhamu ya kiuchumi ya Khilafah. Dola itamsaidia kila mwanafunzi wa kiume na wa kike kufikia uwezo wake kamili bila ya kujali utajiri wao na kuwasaidia kufika kiwango cha juu zaidi cha usomi na ubunifu ili kuzalisha wingi wa mujtahidina, wanasayansi, na wavumbuzi wa kipekee InshaAllah.  

“Dola hupeana maktaba na maabara na njia zote za elimu nje ya shule na vyuo vikuu, ili kuwawezesha wale wanaotaka kuendeleza utafiti wao katika nyanja tofauti tofauti za elimu, kama fiqh, Hadith na tafsiri ya Qur’an, fikra, utabibu, uhandisi na kemia, uvumbuzi, utambuzi, nk. Hili hufanywa ili kuunda ndani ya Ummah mujtahidina wengi zaidi, wanasayansi na wavumbuzi wa kipekee.” (Kifungu cha 179, Kielelezo cha Katiba ya Al-Khilafah cha Hizb ut Tahrir)

• Katika ruwaza ya Khilafah ya Elimu ya Juu, kuna ndoa ya karibu baina ya nidhamu ya elimu ya dola na utekelezaji mahitaji ya mujtamaa. Kwa mfano, mojawapo ya malengo ni kuimarisha shakhsiya ya Kiislamu ya wanafunzi wa elimu ya juu ili kuwafanya kuwa viongozi wanao linda na kutumikia kadhia nyeti za Ummah, kama vile kuhakikisha utabikishaji sahihi wa Uislamu, kuuhisabu uongozi, kubeba ulinganizi, na kupambana na matishio ya umoja wa Ummah, Dini au Khilafah. Hii yamaanisha kuwa thaqafa ya Kiislamu inafundishwa kwa njia ya kuendelea kwa wanafunzi wa elimu ya juu, bila ya kujali taaluma zao walizo chagua. Khilafah pia itashajiisha na kutoa njia za wanafunzi kuchukua taaluma katika nyanja zote za thaqafa ya Kiislamu ili kuzalisha wanazuoni, viongozi, makadhi na mafuqaha wa dola wa siku za usoni ili Ummah uendelee katika utabikishaji, kuhifadhi, na kueneza Dini yao.

• Elimu ya juu pia inatafuta kuzalisha majopo kazi yaliyo na uwezo wa kuchunga maslahi nyeti ya Ummah kama vile kuhifadhi chakula bora na cha kutosha, maji, makao, usalama na matibabu kwa watu, pamoja na kuzalisha madaktari, wahandisi, walimu, wauguzi, wakalimani na wataalamu wengine wa kutosha ili kuchunga mambo ya Ummah. Hili litajumuisha uzalishaji wa wajuzi ambao watachora mipango ya muda mfupi na muda mrefu na kubuni njia na mbinu za kisasa kwa ajili ya maendeleo ya ukulima, viwanda na usalama ili kuiwezesha dola kujitosheleza yenyewe katika kusimamia mambo yake.

• Hivyo basi nidhamu ya elimu ya Khilafah itakuwa ya kipekee, maridadi na isiyo mithili katika umbile lake. Hakika, nidhamu hii ya Kiislamu iliyozaa viongozi wa ajabu kama vile Umar bin Al-Khattab (ra), Umar bin Abdul Aziz, na Harun al Rashid; na wanazuoni wa kipekee kama vile Ash-Shafi, Ibn Taymiyyah, na Nafissa bint Hassan (rm); na wanasayansi maarufu kama vile Ibn Sina, Al-Khwarizmi, na Mariam Al-Astrolabiya’ Al-Ijliya – kwa mara nyengine tena itazaa viongozi, mujtahidina, na wabunifu wa kisayansi wa kipekee kwa Ummah huu inshaAllah – ikizalisha kizazi na hadhara ya dhahabu.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 26 Aprili 2020 10:42

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu