Alhamisi, 09 Shawwal 1445 | 2024/04/18
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Ni Khalifah Pekee Anayejibu Mahitaji ya Wanawake wa Kiislamu

(Imetafsiriwa)

Ushauri (Shurah) na kuhisabu zote ni amri za Mwenyezi Mungu (swt), na miongoni mwa kanuni za hukmu ya Kiislamu, na ni wajibu kwa Khalifah. Kuaminiana kati ya mtawala na raia wake kunahakikishwa kupitia mtawala kuchukua ushauri na mtawala kuhesabiwa na raia wake. Hata hivyo, kwa kuondolewa kwa Khilafah, Waislamu wamenyimwa chanzo hiki cha nguvu, uaminifu na mamlaka. Kito chetu hiki, kilibadilishwa kwa nidhamu duni, mbovu na potofu inayoitwa demokrasia, iliyozaliwa  na akili fisadi. Chaguzi za kidemokrasia na mabunge zilidaiwa kuwa zinatokana na Uislamu, zikifananisha na hukmu ya Kiislamu ya Shurah na uwajibikaji. Walidai kuwa mwanamke wa Kiislamu alionewa, alinyamazishwa na kuchukuliwa kuwa ni sehemu isiyo na natija katika jamii katika karne za Khilafah. Badala yake walimuahidi kuwa na ufanisi na ushawishi katika kuunda nchi zao, watu na ulimwengu kwa njia ya demokrasia ya Kimagharibi.

Hakika, tunaona kwamba wanawake wachache wa Kiislamu, wanaoinuka kuzungumza kwa neno "demokrasia" wakilingania fikra na mifumo ya Urasilimali, wanapewa haki ya kuzungumza katika nchi za Kiislamu, katika Umoja wa Mataifa, katika vyombo vya habari na mabunge ya Amerika au nchi yoyote ya kibepari yenye uadui na Uislamu. Waliweka kundi la watu wasio na akili na wasio na utu karibu nao ili kuunda udanganyifu kana kwamba wanaweza kushawishi watu. Kiasi kwamba hata wao wenyewe wanashangazwa na taswira yao halisi. Jambo kuu ni, wakati baadhi ya wanawake hawa wa Kiislamu wa kidemokrasia wanapewa nyadhifa, ​​vyeo, ​​na tuzo, na kuonyeshwa kama wanawake imara na wenye vivumishi kama vile "mwanamke wa mwaka, watu 100 wenye ushawishi mkubwa zaidi duniani" kwenye jalada la majarida na kusifiwa kama vielelezo, wanaamini kuwa wamepata mafanikio ya kweli. Lakini, wanachofanya ni utekelezaji wa neno moja kwa moja wa orodha ya majukumu waliyopokea na washauri wao wa Kimagharibi. Kwa hakika hotuba zao zote ziliishia kuwa hewa moto na kauli mbiu tupu, huku zikishindwa kuboresha maisha ya wanawake wa Kiislamu. Hawaoni wala hawataki kuona kuwa ni mifumo hii ya kidemokrasia ndiyo inayowanyima wanawake wa Kiislamu mamlaka na uwezo wao, na kuwakataza kupaza sauti zao kama Waislamu, badala yake inawapa nguvu wakoloni wanaosababisha matatizo baada ya matatizo. Wale wanaotenda ndani ya muundo wa mfumo wa kidemokrasia hawawezi kutimiza matakwa yoyote ya wanawake wa Kiislamu, isipokuwa kama haya yataafiki watawala na tawala zao. Ndiyo maana hatuoni kamwe watetezi wa demokrasia wakiboresha maisha ya wanawake wa Ummah huu.

Ama kwa hakika, wanawake wa Kiislamu wanaowalingania watawala wao kutawala kwa mujibu wa sheria za Kiislamu na si kwa mujibu wa demokrasia, wanaswekwa na mifumo ya sheria za kisekula, na hata kufungwa jela. Ni upotoshaji ulioje kuzungumzia uhuru na haki za kidemokrasia za wanawake, huku mabepari wa kikoloni wakiongozwa na Marekani wakivamia ardhi zetu na kuzigeuza kuwa viwanja vya vita, kuiba mali zetu na kutia sumu akili za vijana wetu kwa thaqafa zao, yote ikiwa ni kwa kisingizio cha kuwakomboa wanawake wa Kiislamu kwa demokrasia... Huku wengine wakipongezwa kwa kutukuza demokrasia na uhuru, wanawake wa Kiislamu, wanaoyaomba majeshi ya Waislamu kuokoa heshima zao, maisha yao, ardhi zao, na wanaoulingania umoja kwa Umma wanatangazwa kuwa magaidi... Kwa hakika, wale wanawake wa Kiislamu wanaoelezea waziwazi matamanio ya wanawake wengi wa Kiislamu, na wanaodai suluhisho la matatizo yao kama inavyotarajiwa na Uislamu, hawanyimwi tu sauti kwenye vyombo vya habari vya mifumo ya kisekula ya kidemokrasia, wananyimwa haki yao ya kuzungumza na watawala wao. Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa fahamu za demokrasia, "kushauri na kuhisabu" zinatumika kuasisi kila aina ya haramu, kuhujumu mfumo wa maisha ulioamriwa na Mwenyezi Mungu, na kuuondoa katika uwanja wa maisha!

Hata hivyo, chini ya utawala wa Kiislamu wa Khilafah, ambao ni aina ya utawala kama ilivyoainishwa kwa Waislamu na Mwenyezi Mungu, neno la mwanamke lina thamani halisi. Uislamu unamlazimu mtawala wa Waislamu, Khalifah, kukidhi mahitaji ya kila mwanachama wa Ummah. Kwa ajili hiyo, Yeye (swt) anamuamuru kushauriana na Waislamu na kuwawajibisha Waislamu kumhisabu mtawala wao. Katika Dola ya Khilafah, kazi hii muhimu itatekelezwa ndani ya Majlis ya Ummah. Baraza la Ummah (Majlis al-Ummah) ni mkusanyiko wa watu binafsi wanaowakilisha mambo ya Waislamu, ili Khalifah aweze kuwaregelea juu ya haya. Wawakilishi hawa huchaguliwa na Ummah ili waweze kutoa malalamiko yao kuhusiana na vitendo vya kidhalimu vinavyofanywa na watawala au matumizi mabaya ya sheria za Kiislamu. Kila raia aliyekomaa na mwenye akili timamu wa Dola, mwanamume na mwanamke, Muislamu au asiyekuwa Muislamu, ana haki ya kuwa mwanachama wa Majlis al-Ummah. Maoni na ushauri wao juu ya vitendo na mambo ya kivitendo yanayohusiana na usimamizi wa mambo ya ndani, kama vile mambo ya utawala, elimu, afya, na uchumi, viwanda, kilimo na mengineyo Khalifah anafungika nayo. Kwa hakika, pale Khalifah anapotaka maoni yao juu ya masuala haya, hana budi kuchukua maoni ya walio wengi. Katika mambo yote haya, neno la mwanamke wa Kiislamu lina nguvu sawa kwa sawa na neno la mwanamume.

Hizb ut Tahrir ilibainisha jambo hili katika maelezo yake yote katika Rasimu ya Katiba ya Dola ya Khilafah - Ibara ya 105 hadi 111 - pamoja na dalili zake za Kiislamu. Wanawake wa Kiislamu wataweza tu kueleza mawazo na hisia zao za Kiislamu, na mahitaji yao, na kudai vitendo kwa mujibu wa radhi za Mwenyezi Mungu (swt) ndani ya mfumo wa Kiislamu, unaotabikishwa chini ya Khilafah. Hapo, sauti yao ndipo itapata mawasiliano ya kweli na utekelezwaji katika uwanja wa maisha, kwani itakuwa inamfunga mtawala.

Mahali pekee, ambapo tunaweza kuishi maisha yanayolingana na radhi za Mola wetu, ni Dola ya Khilafah. Ni Dola ya Khilafah tu, ambapo tunaweza kuwa kina mama, wake, mabinti, na wanasiasa wenye ushawishi mkubwa. Mfumo mwengine wowote huwalaani wanawake wa Kiislamu na wasiokuwa wa Waislamu kwa kuwaweka hatarini ya ukatili unaotokana na akili na matamanio ya wanadamu.

 (أَفَحُكْمَ الْجَاهِلِيَّةِ يَبْغُونَ وَمَنْ أَحْسَنُ مِنَ اللّهِ حُكْمًا لِّقَوْمٍ يُوقِنُونَ)

“Je, wao wanataka hukumu za Kijahiliya? Na nani aliye mwema zaidi katika kuhukumu kuliko Mwenyezi Mungu kwa watu wenye yakini?” [Surah al-Maidah: 50].

 #YenidenHilafet         #ReturnTheKhilafah              #الخلافة_101     #أقيموا_الخلافة

#TurudisheniKhilafah

 Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Zehra Malik

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu